Papa Francisko akumbuka waathiriwa wa mafuriko nchini Mexico
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, Dominika tarehe 19 Septemba 2021, mara baada ya tafakari ya Neno la Mungu na Sala ya Malaika wa Bwana, ameonesha ukaribu wake na maombi kwa ajili ya waathirika wa mafuriko yaliyoikumba Serikali ya Hidalgo, nchini Mexico, hasa wagonjwa waliokufa katika Hospitali ya Tula na familia zao.
Maombi kwa wafungwa katika nchi za kigeni: Papa Francisko akiendelea amewahakikishia sala zake watu mbao wamefungwa pasipo haki katika nchi za Kigeni. “kwa bahati mbaya zipo kesi nyingi kwa sababu tofauti na wakati mwingine ngumu. Ninatumaini kwamba, katika utimilifu wa haki, watu hawa wataweza kurudi katika nchi zao haraka iwezekanavyo”, amesema Papa.
Papa Francisko katika salamu zake pia amewasalimu watu wa Roma na mahujaji wote kutoka nchi mbali mbali, wakiwemo wapoland, Waslovakia, hasa kwa kuzingatia ziara yake ya hivi karibuni nchini humo, Honduras, familia, makundi, vyama na wengine watu binafsi. Kwa namna ya pekee amewasalimia kundi la wanakipaimara kutoka Scandicci na chama cha Wafuasi wa Mtumishi wa Mungu Padre Gianfranco Maria Chiti, Ndugu Mdogo Mkapuchini ambaye anakumbukwa kwa miaka 100 tangu kuzaliwa kwake.
Wazo la Papa Francisko limewandea vie vile waamini waliokusanyika katika Madhabahu ya La Salette, nchini Ufaransa, kwa kukumbuka miaka 175 tangu alipotokea Mama Maria ambaye alionesha machozi kwa vijana wawili. Papa amesema: “Machozi ya Maria yanafanya kufikiria yale ya Yesu akililia Yerusalemu na uchungu wake huko Getsemani ambapo ni kielelzo cha uchungu wa Kristo kwa dhambi zetu na mwaliko ambao daima ni wa sasa wa kujikabidhi katika huruma ya Mungu. Papa amehitimisha kwa kuwatakia Dominika njema na ameomba wasisahau kusali kwa alili yake.