Tafuta

2022.04.01 Papa alizungumza na Uwakilishi wa Watu asilia wa Canada. 2022.04.01 Papa alizungumza na Uwakilishi wa Watu asilia wa Canada.  (Vatican Media)

Ziara ya Kitume ya Papa Francisko nchini Canada,Julai 24-30

Kwa mujibu wa Msemaji wa vyombo vya habari mjini Vatican,Dk.Bruni akizungumza na waandishi wa habari, amethibitisha kuwa baba Mtakatifu atafanya ziara yake ya kitume nchini Canada kuanzia tarehe 24-30 Julai.

Na Angella Rwezaula - Vatican,

Ijumaa tarehe 13 Mei 2022, Msemaji wa Vyombo vya habari Dk. Matteo Bruni, kwa waandishi wa habari juu ya matarajio ya ziara hiyo amesema: “Kwa kupokea mwaliko kutoka Mamlaka ya  raia na Kikanisa na Jumuiya za Watu wa Asili, Baba Mtakatifu Francisko atatimiza Ziara ya Kitume nchini Canada kuanzia tarehe 24 hadi 30 Julai ijayo kwa kutembelea mji wa Edmonton, Québec na Iqaluit.” kwa kuongeza Msemaji wa Vyombo vya habari Vatican amebainisha kwamba "ratiba kamili na maelezo zaidi ya safari hiyo vitatolewa kwa wakati kwa juma zijazo". 

Maumivu na aibu ya siku za nyuma

Katika mkutano na watu wa Asilia hivi karibu, Papa alirudia maneno ya kuomba msamaha kwa yale yaliyokuwa yametokea huko nyuma na kuibuka tena katika nyakati za hivi karibuni baada ya  kwa kwa kaburi la halaiki katika Shule ya Makazi ya Kamloops ya Hindi. Historia ya unyanyasaji iliyotekelezwa kati ya mwisho wa karne ya 19 na miongo ya mwisho ya karne ya 20, wakati serikali ya Canada ilikuwa imeanzisha shule za bweni ili kuingiza watoto wa kiasilia. Shule hizo zilikabidhiwa kwa Makanisa ya Kikristo mahalia  yakiwemo hata lile la Kikatoliki. Katika vituo hivyo ambavyo havina ufadhili wa kutosha, watoto mara nyingi walinyanyaswa na kuteseka.

Uchungu wa Papa

Papa aliwambia kwamba “Najisikia aibu, uchungu na fedheha kwa nafasi ambayo Wakatoliki mbalimbali hasa wenye dhamana ya elimu walifanya katika kila jambo ambalo limewahumiza, katika manyanyaso na kutoheshimu utambulisho wenu. utamaduni wany na hata maadili yenu ya kiroho. Haya yote ni kinyume na Injili ya Yesu.

Njia ya ukweli ya upatanisho

Ziara ya Papa ni moja ya hatua hiyo ya  njia ya upatanisho iliyoanzishwa na Kanisa la Canada, mara baada ya ukweli kujulikana. Njia ambayo Papa Francisko aliawaalika kuchukua kwa sababu mchakato madhubuti wa ukarabati unahitaji hatua madhubuti zaidi. Hivyo kutiwa moyo kuendelea kuchukua hatua kwa ajili ya utafutaji wa uwazi wa ukweli na ili kuhamasisha uponyaji wa majeraha na upatanisho na kuruhusu ugunduzi na kuhuishwa kwa utamaduni wa watu wa kiasilia, kuongeza upendo, heshima yao, uangalifu maalum kwa wao na mila na tamaduni zao.

13 May 2022, 16:58