Maaskofu wa Kenya waweka wakfu nchi chini ya Ulinzi wa Mama Maria
Na Sr. Christine Masivo, CPS – Vatican.
Ibada ya Ekaristi iliyoongozwa na Askofu Mkuu Anthony Muheria wa Jimbo Kuu Katoliki la Nyeri, iliwaunganisha Maaskofu kutoka nchini kote Kenya, mapadre, watawa na wamini waliojimuika katika Misa hii Takatifu kwa sala, tafakari, na kujitolea upya kwa ajili ya ujenzi wa taifa. Misa hiyo ilifayika kunako tarehe 5 Oktoba 2025.
Kenya kuwekwa wakfu chini ya ulinzi wa Maria, Mama wa Mungu
Baada ya sala ya kwanza ya Misa Takatifu, Askofu Mkuu Maurice Muhatia wa Jimbo kuu la Kisumu, na Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Kenya, aliongoza sala ya kuweka nchi ya Kenya wakfu chini ya ulinzi wa Maria, Mama wa Mungu. “Maria ni muombezi wetu, na hii ni kielelezo cha imani yetu kubwa katika nafasi ya mama Maria kama Mama wa Kanisa na Malkia wa Amani,” alisema askofu Muhatia. Waamini wote waliombwa kutafuta ulinzi wa Maria na nuru ya Mungu katikati ya giza, ufisadi, na ukosefu wa haki katika taifa, wakiomba kupitia maombezi ya Maria kwa mwongozo bora na uongozi wa kimungu, na pia kukuza roho ya uadilifu na dhamiri ya kijamii kati ya watu.
Zawadi ya barua ya kichungaji kwa vijana
Kabla ya misa Askofu Mkuu Muhatia, alisoma kwa ufupi barua ya kichungaji kutoka Baraza la Maaskofu katoliki nchini Kesha kwa vijana, yenye mada "Wahusika wakuu wa Matumaini." Vijana waliombwa kusimama na kumweka Mungu kama msingi wa Maisha yao, kwa matumaini na imani. Barua hiyo iliakisi mada za utambulisho katika Kristo, ujasiri wa kimaadili, kutokata tamaa na kuwa na tumaini, hasa matumiani katika nchi ya Kenya, uadilifu wa maadili na uinjilishaji wa kidijitali.
Vijana waige mfano wa Mtakatifu Carlo Acutis
Maaskofu wa Kenya waliwapa mfano wa Mtakatifu Carlos Acutis, aliyetangazwa Mtakatifu hivi karibuni Papa Leo XIV kama mfano wa utakatifu wa ujana. Akinukuu maneno ya Papa Leo wakati wa misa Takatifu akikumbuka maneno ya Mtakatifu Mpya alisema kwamba: “kila mtu huzaliwa asili lakini hufa kama nakala.” Na kwa hiyo maneno haya kwa vijana : “tunajivunia ninyi kuwa watu asili katika Kanisa na si nakala, natunawahimiza msimame kidete katika misingi ya matumaini, Imani na kama mahujaji wa matumaini wenye hatima safi ya mbinguni.” “Vijana ni ishara mpya za ulimwengu na taifa kama mashahidi wa imani, bado mmesalia kuwa ishara ya tumaini; mtafuteni Kristo kuwa msingi wenu,” aliwakumbusha “Mt. Carlo Acutis alikuwa kijana mdogo, na maisha yake yanathibitisha kwamba utakatifu unawezekana katika umri wa ujana.”
Barua hiyo ilitokana na mada kuu tano: utambulisho katika Kristo, kukutana na Kristo katika Maisha yetu, ujasiri, usafi wa moyo na matumaini kwa nchi ya Kenya. “Yesu hakuwa na ubaguzi wa kitamaduni au kidini,” alisema, akiwahimiza vijana “msijiangalie kama washiriki wa makabila au kizazi chao, bali kama zao la pekee wa upendo wa Mungu, uwazi wa moyo, na hekima ya kuishi. "Kila mmoja wenu ni mhusika mkuu wa mabadiliko katika ulimwengu,” alisema. Askofu aliwahimiza vijana kutanguliza familia zao, ili wawe chimbuko la nia ya kujumuisha wengine.
Ujumbe wa matumaini
Wakati wa mahubiri, Askofu Peter Kimani Ndung'u wa Jimbo Embu alisema, "Mungu ameweka hema lake katika nchi yetu kama ishara, kwamba yuko kwa ajili yetu hata katika changamoto mbalimbali tunazopitia." Alisema kujitolea kwa nchi kwa Mama Maria ni ishara kwamba wakenya wana mwombezi. “Kuna tumaini, na tumaini halikatishi tamaa. Tunapaswa kuwa uwepo wa Mungu tunakotoka na ishara ya Mungu kwa taifa kwa wote," askofu aliunga mkono. Askofu Kimani alisisitiza, “Tufanye taifa letu kuwa ishara kwa mataifa yote, ambapo uaminifu, ukweli, uadilifu, upendo, amani na matumaini vinaweza kupatikana kuanzia kwenye mioyo na nyumba zetu.
Mwaliko wa umoja
Askofu aliwaalika vijana kupinga migawanyiko ya kisiasa na kiutamaduni. Tumekusanyika katika imani na kuwa kitu kimoja na kuendeleza mazingira ya pamoja wa kusikilizana na kumsikiliza Roho Mtakatifu anatuambia nini. Alisema kuna haja kubwa ya amani, umoja, na upatanisho katika migawanyiko yote ya Kenya, akisema manufaa ya wote lazima yaafikie maswala finyu, ili yeyote asiachwe nyuma. Upatanisho ni mchakato unaodai unyenyekevu na mazungumzo.