Baraza la Makanisa Ulimwenguni lazindua 'Majuma Saba ya Maji'
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Katika mpango uliozinduliwa na Mtandao wa Maji wa Kiekumeni (EWN) wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni(WCC)ni kuhamasisha majibu na vitendo halisi kwa usambazaji wake wa haki. Maji yana maana kubwa ya kiroho katika utamaduni wa Kikristo kama zawadi kutoka kwa Mungu. Hata hivyo, watu bilioni 2.2 Ulimwenguni kote, hasa wanawake na wasichana, hawana upatikanaji wa maji salama ya kunywa. Kampeni iliyoanza siku Jumatano ya Majivu, tarehe 18 Februari 2026, kwa ibada ya maombi, itaendelea hadi Aprili 1. Wahamasishaji wa mpango wa kiekumeni wanasisitiza tena jinsi ilivyo muhimu, katika wakati huu wa mgogoro wa kiuchumi na kimazingira, kwa Wakristo kutafakari kuhusu rasilimali maji na kutekeleza hatua zinazofaa.
Haki ya Maji
Kwa ajili ya tukio hilo, Mtandao wa Kiekumeni umezindua pia mkusanyiko wa tafakari na rasilimali za kibiblia zilizotolewa kwa matumizi ya maji wakati wa Kwaresima. Ili kuboresha juhudi hizi, na kutoa msaada kutokana na ugumu wa kiuchumi unaoonekana kuathiri sehemu nyingi za dunia, Baraza hilo linapendekeza kuratibu mipango na michango mingi ili kushughulikia kwa kiasi masuala yoyote muhimu yaliyopo. "Haki ya maji," alielezea Dinesh Suna, mkuu wa mpango wa Ardhi, Maji, na Chakula wa WCC na mratibu wa Mtandao wa Maji wa Kiekumeni, kuwa "haiwezi kutenganishwa na haki ya kijinsia. Tunapowaona wanawake na wasichana wakitembea kwa saa nyingi kuchota maji, licha ya kutengwa na maamuzi kuhusu usimamizi wa rasilimali za maji, tunashuhudia ukiukwaji mkubwa wa utu wao ambao Kanisa haliwezi kupuuza. Aliongeza, "tunaalika kutafakari, kuomba, na kuchukua hatua ili kuhakikisha kwamba upatikanaji wa maji ya kunywa unakuwa ukweli halisi kwa watoto wote wa Mungu, hasa wale ambao wametengwa kwa muda mrefu."
Machi 22, ni Siku ya Maji Duniani
Kwa hivyo, "Majuma Saba ya Maji" yanalenga kuongeza uelewa wa Kimataifa wakati wa Siku ya Maji Duniani (iliyoanzishwa na Umoja wa Mataifa mnamo 1992), ambayo itaadhimishwa Machi 22. Ingawa uzalishaji wa chakula unategemea upatikanaji wa maji safi, pia una athari kubwa kwa wingi na ubora wa maji. Kwa hivyo umuhimu wa kupitisha mazoea ambayo ni endelevu iwezekanavyo. Hoja hiyo hiyo inatumika kwa uzalishaji wa nishati, ambayo inahitaji kiasi kikubwa cha maji na huathiri vibaya ubora wake. Kwa hivyo ni muhimu kutengeneza sera jumuishi zinazohakikisha mshikamano katika chaguzi zinazofanywa katika sekta mbalimbali zinazohusiana na rasilimali za maji, hasa wakati ambapo upatikanaji wa maji duniani hauwezi kupuuzwa.
Mada Saba za kila juma wakati wa Kwaresima
Tangu 2008, wataalimungu wengi mashuhuri wa kimataifa wameandika tafakari nyingi kuhusu "majuma Saba ya Maji." Mwaka huu, mada saba za kila juma zitaongoza safari wakati wa Kwaresima: jamii zinazostahimili hali ya tabianchi katika muktadha wa maji, usafi wa mazingira, na usafi (WASH); nguvu na mienendo ya kijinsia katika maeneo yenye uhaba wa maji; Maji ya kunywa kama ustawi wa pamoja; uhalisia wa wanawake wa vijijini; usafi wa mazingira kwa ajili ya heshima katika mifumo ya WASH; udhibiti wa maji katika maeneo ya migogoro; na uhusiano kati ya kilimo na WASH. Tafakari hizi za kibiblia zinapatikana kwenye tovuti ya Mtandao wa Kiekumeni, Juma baada ya Juma, pamoja na mawazo ya kujifunza, kutafakari, na kuchukua hatua, ambayo kupitia kwayo Jumuiya za kitawa na watu binafsi wanaweza kuunda majibu yao wenyewe kwa suala la haki ya maji katika jamii zao mahalia.
Mabadiliko Tabianchi yanaongeza ukosefu wa usawa uliopo na hasa wanawake
Kulingana na Athena Peralta, Mkurugenzi wa Tume ya WCC ya Haki ya Tabianchi na Maendeleo Endelevu, haki ya maji na haki ya hali ya hewa vimeunganishwa sana. "Tunapoingia katika Muongo wa Utekelezaji wa Haki ya Tabianchi, Juma Saba za Maji zinatukumbusha kwamba mabadiliko Tabianchi yanaongeza ukosefu wa usawa uliopo na kwamba wanawake ni miongoni mwa wale wanaobeba mzigo mkubwa zaidi. Kampeni hii," Peralta anabainisha, "inaunganishwa na Mfungo wetu wa Kimfumo wa Dunia kutoka hewa chafuzi, ikionesha jinsi taaluma zetu za Kwaresima zinavyoweza kushughulikia mahitaji ya maji ya haraka na mgogoro wa tabianchi wa muda mrefu." Inatoa tafakari na vitendo vya kibiblia vya kila Juma vinavyolenga tasnia maalum za uchimbaji madini: mafuta ya visukuku, uchimbaji wa mafuta na gesi, uchimbaji madini, uvuvi kupita kiasi na ukataji miti, kilimo kwa ajili ya viwanda , na uchimbaji madini wa baharini.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here