2026.02.14:Poland:Historia ya SrDulcissima (Helena) Hoffmann Shirika la Masista wa Maria Asiye na Dhambi 2026.02.14:Poland:Historia ya SrDulcissima (Helena) Hoffmann Shirika la Masista wa Maria Asiye na Dhambi 

Poland:Ujumbe wa kiroho kwa miaka 116 ya kuzaliwa kwa Sr Dulcissima

Mnamo tarehe 7 Februari 2026,watu walikusanyika kusherehekea miaka 116 ya kuzaliwa kwa Mtumishi wa Mungu Helena Hoffmann,anayejulikana Sr Maria Dulcissima.Alizaliwa huko Świętochłowice-Zgoda mnamo 1910 na akafa akiwa na miaka 26.Maisha yake mafupi yalikuwa ushuhuda mkubwa wa upendo uliounganishwa katika msalaba wa Yesu Kristo na urithi wake unawatia moyo wengi wanaotafuta maana katika mateso na uaminifu kwa Mungu.

Na Angella Rwezaula na Sr Christine Masivo,CPS – Vatican.

Maadhimisho ya miaka 116 ya kuzaliwa kwa Mtumishi wa Mungu Sr Maria Dulcissima mwaka huu 2026, yalikuwa wakati wa sala maalum na shukrani. Sherehe hizo zilihudhuriwa na watoto wengi, ambao walimkabidhi nia zao kwa urahisi na furaha, pamoja na watu waliounganishwa kiroho na Sr Maria Dulcissima: watawa, waamini walei na wale ambao wamepata neema kupitia maombezi yake. Sala ya pamoja ikawa usemi wa kumbukumbu hai ya urithi wake wa kiroho na ombi la kutangazwa kwake mwenyeheri haraka.

Maadhimisho ya Miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Maadhimisho ya Miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Maadhimisho ya miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Maadhimisho ya miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima

Maisha yake

Helena Hoffmann alizaliwa huko Zgoda(Eintrachthütte), leo hii ni Wilaya ya Świętochłowice, katika Jimbo Kuu la Katowice nchini Poland, mnamo tarehe 7 Februari 1910 katika familia ya mafundi chuma. Kutoka nyumbani kwa mama yake Msisilesia, akionesha kujitolea kweli, alirithi imani ya kina, mtazamo wa Kikristo, na unyeti maalum kwa kazi na mateso ya wanadamu. Alikuwa ni mtoto wa kwanza kwa Albina na Jòsef Hoffmann.

Baba yake alikuwa mjuzi wa lugha ya Silesian, Kijerumani, na Kipoland, na mama yake alikuwa mzawa wa Kipoland. Tangu utotoni, Helena alikuwa na vipaji vingi na alivithamini vyote kwa roho ya furaha. Alizungumza vema lugha ya Kijerumani na Kipoland na alikuwa mwerevu shuleni na katika klabu ya maigizo. Kujitolea kwake kwa Ekaristi na Bikira Maria kulikuwa na maana ya kina, na alithamini sakramenti.

Mtumishi wa Mungu Sr Maria Dulcissima
Mtumishi wa Mungu Sr Maria Dulcissima

Wito na kujitolea kwake

Tangu utoto wake, mlezi wake wa kiroho, Padre Edward Adamczyk, alimtia moyo wa kumfuasa Kristo kwa ukaribu, kwani Kristo ndiye aliyekuwa kitovu cha maisha yake. Helena alipitia tukio lililoimarisha hisia yake ya kujiunga na maisha ya kitawa, baada ya Komunyo kwanza. Aliokota medali inayoonesha mtawa akiwa ameshika msalaba na waridi, mtu ambaye baadaye alimtambua kuwa ni Teresa wa Lisieux, yaani Mtakatifu Teresa wa Mtoto Yesu.  Mtakatifu Teresa wa Lisieux huyo aliongoza ndoto za Helena na uzoefu wa kiroho, akimtia moyo kusali  na kutoa sadaka kwa ajili ya Kanisa, mapadre na watawa.

Wakati wa Misa ya siku ya kuzaliwa miaka 116 ya  Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Wakati wa Misa ya siku ya kuzaliwa miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima

Helena alijiunga na Shirika la Masista wa Maria asiye na Dhambi(Sisters of Mary Immaculate) mnamo 1927 na mwaka moja baadaye akapokea jina la Maria Dulcissima, "mtamu sana," katika nyumba kuu ya Shirika huko Wrocław nchini Poland. Jina lake lilimaanisha upole wa Kiinjili uliotokana na muungano na Kristo. Alikumbatia mapambano ya ndani ya maisha ya wakfu, chini ya mwongozo wa Padre Josef Schweter CSsR, kwa msaada wa Sr. Maria Lazaria Stephanik, akiongeza sala yake na kukubali mateso kama zawadi. Licha ya magonjwa ya mara kwa mara, dalili zake za kwanza zikionekana kabla ya Noeli ya mwaka 1928, aliendelea kuimarisha maisha yake ya kiroho. Alikuwa wa kiasi na mnyenyekevu kila wakati, amejaa upendo kwa wakubwa wake na masista wenzake, kila wakati akiwa tayari kwa huduma na maombi.

Msalaba, Njia ya Upendo

Kwa njia hiyo maisha ya Sr. Dulcissima yaligubikwa na ugonjwa baada ya kufunga nadhiri zake za kwanza. Aliugua akiendelea kukaa kitandani na hii ikawa shule yake ya siri ya utakatifu, ingawa kupitia macho ya kibinadamu hii inachukuliwa kama mkasa kwa mtawa mdogo mwenye nguvu. Mateso yake yalizidisha maisha yake ya kiroho. Alijitolea maumivu yake kwa ajili ya Mapadre, wenye dhambi, Kanisa, na Shirika lake. Mwili wake ulidhoofika siku baada ya siku, lakini alikuwa na amani na mwanga wa ajabu uliong'aa kutoka katika mwili wake dhaifu. Kitanda chake kikawa altare  yake, na ukimya wake ukawa maombezi.

Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima alikuwa na ibada na Mtakatify Teresa wa Mtoto Yesu
Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima alikuwa na ibada na Mtakatify Teresa wa Mtoto Yesu

Mnamo mwaka 1933, alifika Brzezie kwenye Mto Odra, ambapo miaka miwili baadaye alifunga Nadhiri zake za amwisho katika kikanisa cha Konventi yao. Huko, mateso yake yaliongezeka. Hata hivyo, aliendelea kuwatembelea wagonjwa, akihamasisha sifa za wale walio karibu naye kwa maisha yake ya kujitolea kweli. Alitoa mateso yake, akiwa ameungana na yale ya Kristo Mwokozi pekee. Inasemekana kwamba Sr Maria Dulcissima alipokea neema ya madonda, alama za majeraha ya Kristo mikononi mwake, miguuni, na moyoni, akifunga ushirika wa fumbo hili katika mateso. Alikubali kwa njia hiyo toba kwa ajili ya dhambi za wengine, kama tulivyoeleza hapo awali. Sala yake ilikuwa yenye joto: "Nafsi yangu, Yesu, nipe roho." Upendo wake kwa Kanisa haukuyumba, na alimwombea Baba Mtakatifu, Wakristo walioteswa, na ulimwengu uliopotea. Aliona mateso ambayo yangeikumba Ulaya, lakini jibu lake halikuwa na hofu kamwe, bali uaminifu mkubwa zaidi.

Kaburi la Mwenyeheri Sr M.Dulcissima
Kaburi la Mwenyeheri Sr M.Dulcissima

Uaminifu wake

Mnamo tarehe 18 Aprili 1935, Sr Maria Dulcissima alifunga nadhiri zake za daima na akafa mwaka mmoja baadaye tarehe 18 Mei 1936 huko Brzezie nad Odrą akiwa na umri wa miaka 26 tu, kwa amani, huku akiamini Huruma ya Mungu alikubali mwisho wa Mapenzi ya Mungu na kuzikwa katika Makaburi ya zamani ya Kanisa la Parokia. Wakati wakati wa uhai wake, alifurahia heshima kubwa na kuwaheshimu waamini. Kwa sababu ya utakatifu wake ulioonekana, kuheshimiwa mara tu baada ya kifo chake kwa maneno ya ibada ya hiari. 

Waamini wa Parokia, watoto na watawa katika kaburi la Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Waamini wa Parokia, watoto na watawa katika kaburi la Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima

Waamini wa eneo hilo walikusanyika kwa wingi, wakiamini kwamba mtawa huyo aliyekufa alikuwa ni Mtakatifu. Walichukua hata udongo kutoka kaburi lake, wakiamini kwamba ungelinda familia na nyumba zao. Hadi leo hii watu wa Brzezie, pamoja na wale wa parokia zinazozunguka, wanashuhudia neema nyingi zisizohesabika zilizopatikana kutoka kwa Mungu kupitia maombezi yake. Watoto wengi, vijana, na watu wazima, wanaosali kwenye kaburi lake, wanamkabidhi Mungu matatizo ya maisha yao, hasa kwa wagonjwa na wale walio katika matatizo. Mabaki yake yalifukuliwa mwaka 2000 na kuwekwa kwenye jeneza karibu na Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Matayo na Mathias.

Kumbukizi ya kuzaliwa kwa Mtumishi wa Mungu Sr M. Dulcissima.
Kumbukizi ya kuzaliwa kwa Mtumishi wa Mungu Sr M. Dulcissima.

Kumbukumbu ya maisha ya ajabu ya Sr Maria Dulcissima inaendelea milele. Maua kwenye kaburi lake hayanyauki, taa hazizimiki kamwe. Sala yake ya kuamini na imani ya ufanisi wa maombezi yake kwa Mungu hubaki. Mchakato wake wa kutangazwa Mtumishi wa Mungu kuwa mwenyeheri ulianza mwaka 1999 na kukamilika mwaka 2019, huku mchakato wa Vatican ukiendelea. Kwa sasa Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima amekuwa mwombezi mwenye nguvu.

Tumaini kwa wakati wetu

Kwa njia hiyo hata mwaka huu  2026 kama ilivyo kawaida, sherehe ya miaka 116 iliadhimishwa tarehe 7 Februari, ambapo wengi walikusanyika kuomba kupitia maombezi ya Sr. Dulcissima, uwepo wao ukishuhudia urithi wake wa kiroho ambao unabaki hai. Sr. Dulcissima alitoa ushuhuda kinyume na mazoea, akifundisha kwamba utakatifu hautegemei mafanikio ya ajabu yanayoonekana kwa ulimwengu lakini pia huzaliwa katika uaminifu katika kusema: "tazama mimi hapa" kila siku, tunayosema kwa Mungu hata kupitia machozi.

Wasista wa Shirika la Maria Asiye na Dhambi wakiadhimisha siku ya Kuzaliwa kwa Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Wasista wa Shirika la Maria Asiye na Dhambi wakiadhimisha siku ya Kuzaliwa kwa Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima

Maisha yake bado yanang'aa huku neema ikibadilisha uhai wake mfupi uliofichwa kuwa nuru inayong'aa. Kivuli cha msalaba kinatukumbusha kwamba maisha ya kweli ya Kikristo si kutokuwepo kwa mateso, bali ni upendo unaothibitika kuwa na nguvu kuliko hayo. Sr. Dulcissima, ni shahidi mtulivu, ambaye anaendelea kutuelekeza mbinguni, akitualika kuamini, kuvumilia, na kupenda bila kipimo.

Maadhimisho ya Miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima
Maadhimisho ya Miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr Dulcissima

Sala ili aweze kutangazwa Mwenyeheri mtumishi wa Mungu Sr Maria Dulcissima Hoffmann

Mungu, Baba wa huruma, uliupatanisha ulimwengu na nafsi yako kupitia kifo cha Msalabani na Ufufuko wa Mwanao mpendwa Yesu Kristo. Unawaita waamini wote kuunganisha mateso yao na Mateso ya Mwokozi kwa ajili ya mema ya Mwili wake, ambao ni Kanisa. Upokee, kama sadaka yenye harufu nzuri, maisha ya unyenyekevu ya mtumishi wako, Sr Maria Dulcissima; maisha yaliyowekwa alama ya msalaba wa kila siku. Ujitoe kumfunika katika utukufu wa wenyeheri katika ufalme wako, na kwa neema usikie maombi ya watu wako wanaokugeukia kwa ujasiri kwa ajili ya maombezi yake. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.

Maadhimisho ya miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu  Sr M. Dulcissima
Maadhimisho ya miaka 116 ya Mtumishi wa Mungu Sr M. Dulcissima

Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here

 

 

17 Februari 2026, 14:25