Ziara ya Papa Leo XIV nchini Camerun yaakisi mgogoro mzito wa kanda mbili zinazokinzana
Na Sr. Christine Masivo, CPS – Vatican.
Mgogoro wa Kanda inayozungumza Kiingereza nchini Cameroon ulianza kati ya mahakimu na walimu walipopinga uteuzi wa majaji wa kifaransa katika maeneo yao na kisha kukawa na ukandamizaji wa serikali dhidi ya maandamano hayo ambao ulizidisha mvutano wa haraka, na kusababisha machafuko makubwa.
Mizizi ya kikoloni na migawanyiko inayoendelea
Asili ya mgogoro wa Kanda inayozungumza Kiingereza inaanzia nyuma kwenye historia ya ukoloni ya Cameroon. Hapo awali ilikuwa Koloni la Kifalme la Ujerumani, ambapo nchi hiyo iligawanywa kati ya mamlaka ya Uingereza na Ufaransa baada ya Vita vya Kwanza vya Dunia. Ingawa eneo linalozungumza Kifaransa lilipata uhuru mwaka 1960, Eneo linalozungumza Kiingereza lililifuata mwaka 1961, baadaye likachagua kupitia kura ya maoni kujiunga na upande wa Kifaransa. Muungano huo uliunda shirikisho dhaifu ambalo lilijaribu kuziba tofauti za lugha na utawala. Hata hivyo, kukomeshwa kwa utawala wa shirikisho mwaka 1972 kwa ajili ya serikali kuu kulizidisha hisia za kutengwa miongoni mwa jamii zinazozungumza Kiingereza, ambazo ziliogopa mmomonyoko wa mifumo yao ya kisheria na utambulisho wa kiutamaduni.
Kuanzia maandamo hadi migogoro ya silaha
Mgogoro huo ulianza mwaka 2016 wakati wanasheria na walimu wa Kiingereza walipopinga uteuzi wa maafisa wa Kifaransa katika maeneo yao. Ukandamizaji wa Serikali dhidi ya maandamano haya ulizidisha mvutano haraka, na kusababisha machafuko makubwa. Kufikia Oktoba 2017, vikundi vya kujitenga vilikuwa vimetangaza uhuru binafsi na kurasimisha matarajio yake ya kujitenga. Kile kilichoanza kama maandamano ya kiraia kilibadilika kuwa mgogoro wa silaha wenye matokeo mabaya. Elimu imekuwa uwanja wa mapambano. Shule, zinazoonekana kama alama za mamlaka ya Serikali na sera ya lugha, zimekuwa zikilengwa mara kwa mara. Utekelezaji wa elimu ya lugha mbili, hasa utawala wa Kifaransa, umechochea chuki, huku watenganishaji wenye msimamo mkali wakipinga kabisa elimu inayoendeshwa na serikali.
Mgogoro naozidi wa Kibinadamu na usalama
Mgogoro huo unaosababisha gharama ya kibinadamu ni ya kushangaza. Kulingana na makadirio vyombo husika vya masuala ya kibinadamu, inabainisha kuwa zaidi ya watoto 700,000 wamelazimishwa kuacha shule, huku zaidi ya watu milioni 1.5 wakihitaji msaada wa haraka. Mamia elfu wameyakimbia makazi yao ndani ya nchi, na makumi ya mamielfu wamekimbilia nchi jirani ya Nigeria. Ghasia hizo pia zimepunguza upatikanaji wa huduma za afya, huku mashambulizi dhidi ya vituo vya matibabu na wafanyakazi wa misaada yakilazimisha mashirika mengi kusimamisha shughuli zao. Wakati huo huo, mgogoro huo umesababisha kuenea kwa shughuli za uhalifu, ikiwa ni pamoja na utekaji nyara kwa ajili ya fidia. Mnamo 2024 pekee, karibia visa 450 vya utekaji nyara vilirekodiwa, vikiwalenga raia, Mapadre, na viongozi wa kijamii.
Ukosefu wa usalama
Inashangaza kwamba hata watu mashuhuri kama vile, Askofu Mkuu Mstaafu Christian Tumi wa jimbo Kuu la Douala, hawakuachwa, na kuonesha ukosefu wa usalama ulioenea. Makundi ya kujitenga yenye silaha mara nyingi hujulikana kama “Amba Boys” pia yametoza kodi haramu kwa wakazi wa eneo hilo, na kuwabebesha mzigo jamii ambazo tayari ziko hatarini. Katikati ya msukosuko huo, Kanisa Katoliki linaendelea kuchukua jukumu muhimu kama mpatanishi asiyeegemea upande wowote.
Askofu Mkuu Andrew Nkea Fuanya wa Jimbo Kuu la Bamenda alisisitiza kujitolea kwa Kanisa katika mazungumzo, kudumisha ushirikiano na vikosi vya serikali na vikundi vya kujitenga katika kutafuta amani. Wakati Papa Leo XIV anajiandaa kuingia katika muktadha huu dhaifu, ziara yake ya Kitume inatarajiwa kuwa na umuhimu si wa kiroho tu, bali pia wito mpya wa upatanisho katika eneo linalotamani utulivu na amani.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata taarifa mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku:Just click here.