Papa atoa wito wa kusitisha mapingano nchini Myanmar:
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Dominika tarehe 19 Oktoba 2025, wakati Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 99 ya Kimisionari na kutangazwa Watakatifu 7 wapya wa Kanisa, mara baada ya misa na kabla ya sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu Leo XIV aliwasalimia kwa moyo wote wale wote walioshiriki “maandhimisho ambayo yamekuwa siku kuu kubwa ya Utakatifu.”
Baba Mtakatifu kadhalika alishukuru Makardinali, Mapatriaki, na Maaskofu waliokuwapo; kama vile hata salamu na utambuzi wa Rais wa Jamhuri ya Italia, Bwana Sergio Mattarella, Rais wa Lebanon, na Wawakilishi rasmi kwa namna ya pekee wa Armenia na Venezuela.
Papa Leo XIV aliwakaribisha kwa furaha mabinti wa kiroho wa Waanzilishi waliotangazwa kuwa watakatifu leo hii na jumuiya mbalimbali na vyama vinavyohamasishwa na karama za Watakatifu wapya. “Asanteni nyote kwa ushiriki wenu wa dhati!”
“Ninatoa salamu zangu kwa mahujaji wengine waliohudhuria, hasa Udugu wa Bwana wa Miujiza, walioadhimisha maandamano yao.”
Siku ya kimisionari
Papa Leo kadhalika alisema “Leo ni Siku ya Utume wa kimisionari Duniani. Kanisa ni la kimisionari kabisa, lakini leo hii tunawaombea hasa wale wanaume na wanawake walioacha kila kitu kwenda kuwapelekea Injili wale wasioijua. Ni wamisionari wa matumaini miongoni mwa watu. Bwana awabariki!”
Papa akitazama sehemu nyingine za Ulimwengu wa ghasia alisema: “ Habari zinazotoka Myanmar ni za kusikitisha: zinaripoti mapigano yanayoendelea ya silaha na mashambulizi ya angani, ikiwa ni pamoja na yale yanayoathiri raia na miundombinu. Niko karibu na wale wanaoteseka kwa jeuri, ukosefu wa usalama, na magumu mengi sana. Ninasasisha ombi langu la kutoka moyoni kwa usitishaji mapigano wa haraka na unaofaa. Vyombo vya vita vitoe nafasi kwa wale wa amani, kwa njia ya mazungumzo jumuishi na yenye kujenga!”
“Tukabidhi maombi yetu endelevu kwa ajili ya amani katika Nchi Takatifu, Ukraine, na maeneo mengine yenye migogoro kwa maombezi ya Bikira Maria na Watakatifu wapya. Mwenyezi Mungu awape hekima na subira wote wanaoongoza katika kutafuta amani ya haki na ya kudumu.”
