Papa Leo XIV:Wasiwasi wa Papa kuongezeka kwa chuki dhidi ya Wayahudi duniani
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Mara baada ya Misa, Takatifu na kabla ya kuanza sala ya Malaika wa Bwana Dominika tarehe 5 Oktoba 2025, Baba Mtakatifu Leo XIV aliwageukia umati wa waamini na mahujaji 30,000 waliokusanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Petro akisema kuwa “Ndugu wapendwa, kabla ya kusali Sala ya Malaika wa Bwana, ningependa kuwasalimu na kuwashukuru nyote mlioshiriki katika maadhimisho ya Jubilei hii maalum kwa wamisionari na wahamiaji. Ninyi ni wamisionari wazuri kwa sababu mlikuja hata kwenye mvua! Asante! Kanisa ni la kimisionari kabisa na ni watu mmoja wakuu wanaosafiri kuelekea Ufalme wa Mungu.
“Leo, kaka na dada zetu wamisionari na wahamiaji wanatukumbusha jambo hilo. Lakini hakuna mtu anayepaswa kulazimishwa kuondoka, wala kunyonywa au kudhulumiwa kwa sababu ya hali yake kama mhitaji au mgeni! Heshima ya mwanadamu daima huja kwanza! Nawasalimu mahujaji wote waliohudhuria, hasa wale wa Jimbo la Pavia, wakiongozwa na Askofu; pamoja na waamini, wakiwemo baadhi ya vijana kutoka Bethlehemu, wanaobeba sanamu ya Bikira wa Ufunuo.”
“Jioni ya Jumanne, Septemba 30, tetemeko kubwa la ardhi lilipiga eneo la kati la Ufilipino, hasa mkoa wa Cebu na mikoa jirani. Ninaeleza ukaribu wangu kwa watu wapendwa wa Ufilipino, na hasa ninasali kwa ajili ya wale walioathiriwa sana na matokeo ya tetemeko la ardhi. Tuendelee kuwa wamoja na mshikamano katika kumtumaini Mungu na maombezi ya Mama yake katika kila hatari.”
Papa kadhalika alionesha wasiwasi kwamba “ Ninaelezea wasiwasi wangu kuhusu kuongezeka kwa chuki dhidi ya Wayahudi ulimwenguni kote, kama ilivyoonekana kwa huzuni na shambulio la kigaidi huko Manchester siku chache zilizopita. Ninaendelea kuhuzunishwa na mateso makubwa waliyovumilia watu wa Palestina huko Gaza.”
Hata hivyo, Papa hakuacha kuonesha juhudi zinazoendelea kwamba “Katika saa za hivi karibuni, huku kukiwa na hali ya kutisha katika Mashariki ya Kati, hatua kubwa zimepigwa katika mazungumzo ya amani, ambayo ninatumaini itafikia matokeo yanayotarajiwa hivi karibuni.” Kwa njia hiyo, “ Nninawaomba viongozi wote wajitolee katika njia hii, kusitisha mapigano na kuwaachilia mateka, huku nikiwasihi waendelee kuwa wamoja katika maombi, ili juhudi zinazoendelea ziweze kukomesha vita na kutupeleka kwenye amani ya haki na ya kudumu.”
Bikira Maria wa Rozari huko Pompei
Katika fursa ya Maombi kwa Bikira Maria wa Rozari, Baba Mtakatifu hakusahau kwamba “Tunaungana kiroho na wale waliokusanyika kwenye Madhabahu ya Pompeii kwa ajili ya Sala kwa Bikira wa Rozari Takatifu. Katika mwezi huu wa Oktoba, tukitafakari pamoja na Maria mafumbo ya Kristo Mwokozi, tunazidisha maombi yetu ya amani: sala inayoonesha mshikamano thabiti na watu wanaoteswa na vita. Asante kwa watoto wengi ulimwenguni ambao wamejitolea kusali Rozari kwa nia hii. Asante kwa moyo wote!
Angelus Domini…
Asante sana kusoma makala hii, ikiwa unakata kubaki na masasisho zaidi, tunakualika kujiandikisha hapa: Just click here
