Papa Leo,asali Rozari kuombea amani duniani:Wenye nguvu wawe jasiri kupokonywa silaha
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Siku ambayo ilitarajiwa ya Jumamsoi tarehe 11 Oktoba 2025 kwa ajili ya maombi ya Papa, imewaona waamini kutoka pande za Dunia katika Jubilei ya Tasaufi ya Maria, pamoja na ya Watawa wote ikiwa ni pamoja na, mapadre, watu wa kujitolea kutoka katika madhabahu mbali mbli za Maria duniani, pamoja na washiriki wa harakati za Maria, Mashirika mbali mbali ya Kitawa na vikundi vya maombi, waliokusanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Petro Jumamosi jioni saa 12.00 kusali pamoja Rozari Takatifu katika mkesha wa maombi ulioongozwa na Baba Mtakatifu Leo XIV kama aliyokuwa amewaalika waamini hivi karibuni kusali naye kwa ajili ya kuomba zawadi ya amani, duniani.
Kwa mujibu wa taarifa, za Vatican, mahujaji wapatao therathini elfu walishiriki mkesha huu wa maombi ya kina na Baba Mtakatifu ambayo yalihitimishwa kwa kuabudu Sakramenti Takatifu.
Katika tafakari yake wakati wa Rozari, Baba Mtakatifu Leo XIV aliwaalika waamini kudumu katika sala bila kuchoka kwa ajili ya amani, zawadi kutoka kwa Mungu ambayo tunapaswa kujitahidi kuipokea na ambayo ni lazima kujitolea kwa nguvu zote. “Wakati wa Jubilei hii ya Tasaufi ya Maria sisi wamini tunaelekeza macho yetu kwa Bikira Maria, ambaye anatuongoza katika hija yetu ya matumaini" alisema Papa Kadhalika aliwakumbusha waamini kwamba kujitoa kwa Maria ni halisi zaidi unapojikita ndani ya kuiga maadili ya kibinadamu na ya kiinjili ya Maria, na kwa hiyo aliwaalika kuomba zawadi ya huruma kuelekea kila kaka na dada anayeteseka, na kwa viumbe vyote.
Baba Mtakatifu Leo alikumbuka maneno ya mwisho yenye thamanikumhusu Maria katika Injili inayoeleza Harusi ya Kana ambapo Mama maria alisema kwamba “Fanyeni lolote atakalowaambia.” Kwa njia hiyo kama nuru, Papa aliongeza Maria anajielekeza zaidi yake, akionesha kwamba mwisho wa yote ni Bwana Yesu na Neno Lake. Mama wa Mungu anatualika kuishi Injili, kuiishi kwa dhamira na furaha, tukijua kwamba kwa kufanya hivyo, maisha yetu yatageuzwa kutoka utupu na yasiyo na uchungu hadi kuwa kitu kilichojaa na kuchangamka. Papa alisema, kamwe tusiruhusu maneno Yake yaanguke chini, yaani maneno ya Yesu katika bustani ya Gethsemane, kabla ya Mateso, aliyoeleza mwenyewe kuwa “Weka chini upanga wako.”
Katika hili Papa alisisitiza tena kwamba “amani haina silaha na kupokonya silaha. Si kuzuia bali ni udugu; si kauli ya mwisho, bali mazungumzo. Amani haitakuja kama matokeo ya ushindi juu ya adui, lakini kama tunda la kupanda haki na msamaha wa ujasiri.” Kwa kusisisitiza kuhusu "weka upanga wako chini” Papa alisema kwamba ni ujumbe unaoelekezwa kwa wenye nguvu duniani, kwa wale wanaoongoza hatima ya watu: kuwa na ujasiri wa kupokonya silaha na wakati huo huo, ni mwaliko kwa kila mmoja wetu kutambua kwamba hakuna wazo, imani, au sera yoyote inayohalalisha mauaji ya ndugu.
Ni lazima kwanza tuvunje silaha mioyoni mwetu kwa sababu tusipokuwa na amani ndani yetu wenyewe, hatuwezi kuwapatia wengine.”Baba Mtakatifu aliendelea na tafakari hyake huku akitoa mwaliko kuwa na mtazamo tofauti ili kuona ulimwengu na si katika mtazamo wa wenye nguvu, bali wa walio wadogo ili kuweza kutafakari juu ya matukio ya historia kwa maoni ya mjane, yatima, mgeni, mtoto aliyejeruhiwa, mhamiaji na mkimbizi. Ikiwa hatujifunzi kufanya hivyo, ni kwamba “hakuna chochote kitakachobadilika kamwe,na enzi mpya, ya ufalme wa haki na amani, hataibuka kamwe.”
Kwa kuhitimisha Papa wa Roma alikumbusha heri za Mlimani: “Heri wapatanishi.” Kisha Papa aliomba kusali kwa mama Maria, Malkia wa Amani, huku akimwomba atufundishe kusikiliza kilio cha maskini na dunia na kuishi na kutoa ushuhuda kwa upendo wa Kikristo, kwa kukaribisha kila mtu kama kaka na dada; kuachana na giza la ubinafsi ili kumfuata Kristo, nuru ya kweli ya ubinadamu.
Sala ya Baba Mtakatifu: Tumekusanyika jioni hii katika maombi karibu na Maria, Mama wa Yesu na Mama yetu, kama wanafunzi wa kwanza katika Chumba cha Karamu Kuu. Kwake, mwanamke aliye na amani sana, Malkia wa Amani, tunageukia: Omba pamoja nasi, Mwanamke mwaminifu, tumbo takatifu la Neno. Utufundishe kusikiliza kilio cha maskini na cha Mama Dunia, usikilize mwito wa Roho katika siri ya moyo; katika maisha ya kaka na dada zetu, katika matukio ya historia, katika kuomboleza na kushangilia kwa uumbaji. Maria Mtakatifu, Mama wa walio hai, mwanamke mwenye nguvu, mwenye huzuni, mwaminifu, Bikira-arusi Msalabani, ambapo upendo hukamilika na maisha huchipuka, kuwa mwongozo wa kujitolea kwetu katika huduma. Tufundishe kusimama nawe kwenye misalaba isiyo na kikomo, ambapo Mwanao bado amesulibiwa, ambapo maisha yanatishiwa zaidi; kuishi na kushuhudia upendo wa Kikristo, kuwakaribisha kka au dada katika kila mwanamume; kuachana na ubinafsi mbaya kumfuata Kristo, nuru ya kweli ya wanadamu. Bikira wa Amani, mlango wa tumaini hakika, usikilize maombi ya watoto wako!
