Vatican:"Kuhifadhi Sauti na Nyuso za Binadamu"
Vatican News
Katika kuadhimisha Siku ya 60 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni kwa Mwaka 2026, Baraza la Kipapa la Mawasiliano limeandaa Mkutano wa Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana,Roma siku ya Alhamisi tarehe 21 Mei 2026. Mada itakayoongoza hafla hiyo itakuwa ni: "Kuhifadhi Sauti na Nyuso za Binadamu," ambayo itarudia Kauli mbiu ya Ujumbe wa Baba Mtakatifu Leo XIV kwa ajili ya Siku hiyo, inayosisitiza roho ambayo waandaaji wamewaalika wasomi, wawakilishi wa taasisi, wataalamu wa teknolojia ya hali ya juu, na waandishi wa habari kujadili Akili Unde na athari zake katika maisha ya watu binafsi, jamii, na mataifa.
Hafla hiyo, kwa ushirikiano na Baraza la Kipapa la Utamaduni na Elimu na Mfuko wa Kipapa wa Yohane XXIII, itafanyika kwa siku nzima katika Ukumbi Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana. Tukio hili linalenga kuwa wakati wa kutafakari na kujadiliana, likiitikia wito wa Papa wa "kuhifadhi zawadi ya mawasiliano kama ukweli wa ndani kabisa wa ubinadamu, ambapo uvumbuzi wote wa kiteknolojia unapaswa pia kuelekezwa." Mkutano huo utafunguliwa kwa hotuba za Dkt. Paolo Ruffini, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano, na Kardinali José Tolentino de Mendonça, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Utamaduni na Elimu.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.