Mama Kanisa anaadhimisha Sherehe ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, msingi wa Mafumbo yote yanayosherehekewa na Kanisa kwa nyakati mbalimbali. Mama Kanisa anaadhimisha Sherehe ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, msingi wa Mafumbo yote yanayosherehekewa na Kanisa kwa nyakati mbalimbali.   (@Vatican Media)

Sherehe Fumbo Utatu Mtakatifu: Mungu Mmoja Katika Nafsi Tatu!

Mababa wa Kanisa wanasema, Imani Katoliki ndiyo hii: “Tunamwabudu Mungu Mmoja katika Utatu na Utatu katika Umoja, bila kugawanyika nafsi, wala kutenganisha uwamo; kwani ni Nafsi ya Baba, ya Mwana na Roho Mtakatifu. Ni umungu mmoja wa Baba, na wa Mwana na wa Roho Mtakatifu, utukufu ulio sawa, ukuu wa pamoja wa milele.” KKK 266. Mungu ni Baba wa milele, Mwana ni uwamo pamoja na Baba na Roho Mtakatifu anatoka kwa Baba na Mwana!

Na Padre Octavian O. Hinju, CP- Morogoro, Tanzania

Neema ya Bwana wetu Kristo Yesu, na pendo la Mungu na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote! Mama Kanisa anaadhimisha Sherehe ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, msingi wa Mafumbo yote yanayosherehekewa na Kanisa kwa nyakati mbalimbali. Hili ni Fumbo la imani na la maisha ya Kikristo. Ni Fumbo la Mungu ndani yake Mwenyewe. Mwenyezi Mungu katika historia na Mpango wa ukombozi amejifunua kuwa ni Mungu mmoja katika Nafsi Tatu. Baba Mungu Mwenyezi Mwumba mbingu na nchi, na vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana. Kanisa linasadiki kwa Kristo Yesu, Mwana wa pekee, wa Mungu aliyezaliwa kwa Baba tangu milele yote. Ni Mungu aliyetoka kwa Mungu, Mwanga kwa mwanga. Mungu kweli kwa Mungu kweli. Aliyezaliwa bila kuumbwa, Mwenye umungu mmoja na Baba. Ndiye aliyeshuka kutoka mbinguni kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu. Aliteswa, akafa na kufufuka kwa wafu! Kanisa linasadiki kwa Roho Mtakatifu, Bwana na mleta uzima: atokaye kwa Baba na Mwana. Anayeabudiwa na kutukuzwa na Baba na Mwana: Aliyenena kwa vinywa vya Manabii. Mababa wa Kanisa wanasema, Mwenyezi Mungu amejifunua jina lake linaloelezea uwapo, Umoja wa Nafsi, na maana ya maisha yake na kwamba, jina lake ni kielelezo cha nguvu. Mungu amejifunua jina lake, amejijulisha na kujionesha ili aweze kukaribiwa, kujulikana na kutajwa kwa Nafsi yake. Fumbo la Utatu Mtakatifu ni msingi wa imani na maisha ya Kikristo. Fumbo la Umwilisho linafunua kwamba, Mungu ni Baba wa milele, na Mwana ni uwamo wa pamoja na Baba, yaani ndani yake, na pamoja Naye, ni Mungu mmoja tu.

Roho Mtakatifu anatoka kwa Baba na Mwana ni uwamo wa pamoja!
Roho Mtakatifu anatoka kwa Baba na Mwana ni uwamo wa pamoja!   (@VATICAN MEDIA)

Roho Mtakatifu anatumwa na Baba na Mwana ni uwamo wa pamoja, anaabudiwa na kutukuzwa pamoja na Baba na Mwana. Kwa neema ya Ubatizo, waamini wanaitwa kushiriki Uzima wa Fumbo la Utatu Mtakatifu, hapa duniani katika giza la imani, na baada ya kifo katika Mwanga wa milele.  Mababa wa Kanisa wanasema, Imani Katoliki ndiyo hii: “Tunamwabudu Mungu Mmoja katika Utatu na Utatu katika Umoja, bila kugawanyika nafsi, wala kutenganisha uwamo; kwani ni Nafsi ya Baba, ya Mwana na Roho Mtakatifu. Ni umungu mmoja wa Baba, na wa Mwana na wa Roho Mtakatifu, utukufu ulio sawa, ukuu wa pamoja wa milele.” KKK 266.Katika utangulizi wa Maadhimisho ya Sherehe hii tunasali hivi: “Wewe pamoja na Mwanao wa pekee na Roho Mtakatifu u Mungu mmoja na Bwana mmoja, siyo katika umoja wa nafsi, ila katika Utatu wa Mungu mmoja. Mambo tunayoyasadiki juu ya utukufu wako, kwa sababu ya ufunuo wako, twayasadiki pia juu ya Mwanao na juu ya Roho Mtakatifu pasipo tofauti ya kutengana.” Sehemu hii ya ibada ya Misa Takatifu inatupatia kwa muhtasari maana ya Fumbo hili tunaloliadhimisha. Imani yetu katika Mungu mmoja si umoja wa nafsi bali ni Mungu mmoja katika nafsi tatu, yaani, Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho Mtakatifu.

Kanisa linamwabudu Mungu mmoja katika utatu na utatu katika umoja
Kanisa linamwabudu Mungu mmoja katika utatu na utatu katika umoja   (@Vatican Media)

Ndugu wapendwa wasikilizaji na wasomaji wa Vatican News, hatimaye mara baada ya kipindi cha Pasaka ambacho kilitamatishwa kwa sherehe ya Pentekoste; Liturujia ya Kanisa inatupa mwaliko mwingine wa kuadhimisha sherehe tatu za Bwana; leo, katika Dominika hii ya 9 katika kipindi cha kawaida, Kanisa linaadhimisha Sherehe ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, kwa mujibu wa kalenda ya liturujia Alhamisi ijayo ni Sherehe ya Mwili na Damu lakini kutokana na sababu za kichungaji sehemu nyingi dunia itaadhimishwa Dominika ya tarehe 07 Juni 2026; na mwishowe ni sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu itakayo adhimishwa Ijumaa ya tarehe 12 Juni 2026. Kila moja ya matukio haya ya kiliturujia yanaangazia ukweli ambao fumbo zima la imani yetu Katoliki inafumbatwa. Ukweli huu wa Imani unajengwa kwa njia ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na kiini cha Fumbo la Umwilisho, fumbo linalo tutanabaishia kwa uwazi umungu na ubinadamu wa Kristo. Itakumbukwa kuwa tuliishia juma la saba katika kipindi cha kawaida tukaanza Kipindi cha Kwaresima kwa Jumatano ya Majivu na baadae Kipindi cha Pasaka na baada ya Sherehe ya Pentekoste iliyofunga kipindi cha Pasaka tukaanza wiki ya juma la 8 na Jumapili ya 10 kipindi cha kawaida tutaadhimisha Sherehe ya Ekaristi Takatifu. Kumbe safari hii masomo ya jumapili ya 8, 9 na 10 kipindi cha kawaida mwaka A 2026 hatutayatafakari kwa sababu masomo ya Sherehe hizi yanachukua nafasi yao.

Ni Umungu Mmoja wa Baba na wa Mwana na Roho Mt.; Utukufu ulio sawa
Ni Umungu Mmoja wa Baba na wa Mwana na Roho Mt.; Utukufu ulio sawa   (@Vatican Media)

Ndugu wapendwa wasikilizaji na wasomaji wa Vatican News, Kanisa linafundisha kuwa Utatu Mtakatifu ni fumbo la imani ya kuwa katika Mungu mmoja kuna Nafsi Tatu zisizogawanyika katu yaani Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho. Hizi nafsi tatu za Mungu mmoja, zote ni sawa katika uasili. Utatu Mtakatifu ni moyo na kiini cha imani yetu ya kikristo. Ni fumbo asili la imani na maisha ya Kikristo. Ndiyo maana Misa na sala zote katika Kanisa Katoliki zinaanza na kumalizika kwa maneno haya: “Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu” ambayo ni namna fupi kabisa ya kumkiri Mungu mmoja katika Nafsi tatu. Katika hii sala rahisi namna hii, tunakiri kile tunachokiamini kwa kirefu katika Kanuni ya Imani katika sehemu kuu tatu tunaposali tukisema: “Nasadiki kwa Mungu mmoja Baba Mwenyezi, mwumba wa mbingu na Dunia… Nasadiki kwa Yesu Kristo, Mwana wa pekee wa Mungu, ameshuka toka mbinguni kwa ajili yetu sisi wanadamu na kwa ajili ya wokovu wetu…Nasadiki kwa Roho Mtakatifu, Bwana mleta uzima…” Sisi wenyewe kwa nguvu na mwangaza wa Roho Mtakatifu, tunashirikishwa katika umoja huo wa mapendo ya kimungu kwa sababu katika Ubatizo tumetiwa muhuri usiofutika kwa jina la Utatu Mtakatifu tulipobatizwa kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu muhuri unao thibitishwa pia kwa Sakramenti ya Kipaimara na kuwekewa mikono. Hivyo inatupasa kuwa na umoja na mapendo kati yetu sisi wenyewe na kati yetu na Mungu katika Utatu Mtakatifu.

Kristo Yesu, Mwana pekee wa Mungu aliyezaliwa bila kuumbwa
Kristo Yesu, Mwana pekee wa Mungu aliyezaliwa bila kuumbwa   (@Vatican Media)

Hayati Baba Mtakatiu Benedikto XVI katika sala ya Malaika wa Bwana katika Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican tarehe 07 Juni 2009 akitafakari juu ya fundisho hili la Imani yetu kwa kusema kwamba “Nafsi tatu ambazo ni Mungu mmoja kwa sababu Baba ni upendo, Mwana ni upendo, Roho ni upendo. Mungu ni upendo kamili na wa pekee, upendo safi zaidi, usio na mwisho na wa milele. Mungu haishi katika upweke wa kupendeza bali ni chanzo kisichoisha cha maisha ambacho hutolewa na kuwasilishwa bila kukoma. Kwa kadiri hii tunaweza kutambua uzuri na utakatifu wa kimungu katika viumbe vilivyo umbwa naye.” Kumbe Mungu hagawanyiki, ni yeye yule mmoja katika Nafsi tatu zinazo fanya kazi moja ya upendo yaani kazi ya kumkomboa mwanadamu. Ndugu wapendwa wasomaji na wasikilizaji wa Vatican News, Utatu Mtakatifu ni Sherehe ambayo kwa njia yake tunamkiri na kumtukuza Mungu mmoja anaye endelea kujidhihirisha kwetu kwa nyakati zote katika Nafsi tatu: yaani Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Maadhimisho ya Sherehe ya Utatu Mtakatifu hufanyika Dominika ya kwanza mara baada ya Sherehe ya Pentekoste. Hii ni Dominika inayofuata mara tu baada ya kipindi cha Pasaka kuhitimishwa. Sherehe hii tunayoadhimisha leo ni sherehe inayogusa fundisho kuu juu ya Mungu mwenyewe. Ni sherehe ambayo pengine huleta mkanganyiko miongoni mwa waamini walio wengi. Ndio maana Mt. Thoma wa Akwino alisali akasema hivi “pale unaposhindwa kuelewa basi wewe amini tu.” 

Ni Mungu aliyetoka kwa Mungu, Mwanga kwa Mwanga!
Ni Mungu aliyetoka kwa Mungu, Mwanga kwa Mwanga!   (@Vatican Media)

Utatu Mtakatifu ni fundisho la imani na wakati huo huo ni Fumbo, kwamba Mungu wa kweli na wa pekee ni mmoja katika Nafsi tatu nazo ni Baba, Mwana na Roho Mtakatifu.  Tunaamini juu ya Fumbo la Utatu Mtakatifu kwa sababu Mungu mwenyewe amelifunua. Amelifunua hatua kwa hatua katika historia ya wokovu; tangu katika Fumbo la uumbaji, katika Fumbo la ukombozi wa mwanadamu na katika Fumbo la kumtuma Roho Mtakatifu. Mungu anayafanya haya yote akiongozwa na amri ya upendo. Tutambue kwamba “Katika mpango huu wa ukombozi kila nafsi ya Mungu inatekeleza kazi yake ya pamoja kufuatana na hali yake kama nafsi. Ndiyo maana tunamtaja Baba kama muumbaji, Mwana kama mkombozi na Roho Mtakatifu kama mfariji anayetakatifuza. Hata hivyo hii yote ni kazi ya pamoja ya nafsi tatu za Mungu kwa sababu hizi ni nafsi zenye asili moja na kwa sababu hiyo zina utendaji mmoja ulio sawa” na maisha yote ya kikristo ni ushirika wa kila nafsi ya Mungu bila kuzitenganisha kwa namna yoyote. Anayemtukuza Baba hufanya hivyo kwa njia ya Mwana katika Roho Mtakatifu; anayemfuata Kristo anafanya hivyo kwa sababu Baba anamvuta na kwa sababu Roho Mtakatifu anamwongoza.

Roho Mtakatifu ni Bwana na Mleta Uzima!
Roho Mtakatifu ni Bwana na Mleta Uzima!

Somo la Kwanza ni Kutoka 34: 4b-6, 8-9. Somo hili linatufunulia jinsi Mungu anavyo jidhihirisha kwa Musa kama Mungu wa huruma, neema, na wingi wa wema. Ni katika fadhila hizo, mwanadamu anapewa nafasi ya kuufurahia ukuu na uzuri wa Mungu. Somo la Pili ni 2 Wakorintho 13: 11-14. Paulo Mtume katika Waraka huu, anahitimisha kwa kutoa baraka kuu katika fumbo la Utatu Mtakatifu: anaposema Neema ya Bwana Yesu, upendo wa Mungu Baba, na ushirika wa Roho Mtakatifu. Ni maneno haya ambayo Mama Kanisa huyatumia pia mwanzo mwa adhimisho la Ekaristi Takatifu. Injili ni kama ilivyoandikwa na Yohane 3: 16-18. Yohane Mwinjili anathibitisha upendo mkuu wa Mungu ulimwenguni kwa kumtoa Mwanae wa pekee ili kila amwaminiye awe na uzima. Maandiko Matakatifu yanapozungumza juu ya Fumbo la “Utatu Mtakatifu” yanamrejelea Mungu mwenyewe na utambulisho wake wa kweli. Ni utambulisho unaoangazia uumbaji wote (Mwz. 1:26), ambamo viumbe vyote huishi na kuwa na uhai ndani yake uhai usio na mwisho ambao umetolewa, kwa neno moja tu, nalo ni neno la upendo; “katika yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu” kama Mtume Paulo alivyosema katika Areopago ya Athene (Mdo. 17:28). Huu ni uthibitisho wenye nguvu zaidi kwamba tumeumbwa kwa mfano wa Utatu, na uthibitisho huo ni huu: upendo pekee hutufanya tuwe na furaha kwa sababu tunaishi katika uhusiano, na tunaishi kupenda na kupendwa. Kumbe alama ya kina ya Utatu, wa Mungu ni upendo.

Roho Mtakatifu alinena kwa vinywa vya Manabii
Roho Mtakatifu alinena kwa vinywa vya Manabii

Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, wanalitambulisha Kanisa kama taifa jipya la watu wa Mungu lililo kusudiwa tangu kuumbwa kwa ulimwengu ili liwe chombo cha ukombozi unaokamilika katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Mapendo kati yetu sisi wenyewe yanapaswa yaonekane katika maisha yetu ya kila siku popote pale tulipo tukisaidiana kwa hali na mali, tukiishi kwa umoja, amani na upendo; tukilenga hasa katika kutafuta maisha ya utakatifu (LG. 40). Umoja na upendo kati yetu na Mungu katika Utatu wake, unajidhihirisha katikati yetu kwa njia ya sala ambayo ni moja ya nguzo muhimu sana ya maisha yetu ya kiroho. Sala inaleta umoja na kudumisha uhusiano mzuri na mwenyezi Mungu, kwa hiyo ni muhimu kusali katika familia na katika jumuiya zetu ndogondogo za Kikristo na zaidi sana kushirika katika maadhimisho ya Misa Takatifu. Kumbe, Sherehe hii inatuhimiza tuwe wamoja katika maisha yetu tukisaidiana katika taabu na raha. Tujenge familia zenye umoja thabiti unaosimikwa katika upendo. Ni kutoka katika umoja wa kifamilia ndipo tunaweza kuwa na umoja katika nyanja zingine za maisha yetu na kuishi kwa kupendana.Kwa ujumla wake maadhimisho haya yanatualika kutafakari fumbo la Mungu aliye mmoja katika Nafsi tatu, tunaitwa kuishi kwa upendo, amani, na mshikamano kama familia ya Mungu. Hivyo basi, tumuombe Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho Mtakatifu, watukirimie fadhila ya mapendo katika maisha yetu ili kwa kwapenda wanadamu wenzetu kadhalika tumpende pia Mungu. Mababa wa Kanisa wanasema, familia ya Kikristo katika mpango wa Mungu ni umoja wa watu, ishara na mfano wa umoja wa Fumbo la Utatu Mtakatifu. Kazi ya familia ya uzazi na malezi ya watoto hunurisha kazi ya Baba ya Uumbaji. Familia inaitwa kushiriki sala na sadaka ya Kristo Yesu. Sala ya kila siku na somo la Neno la Mungu huimarisha upendo ndani yake. Familia ya Kikristo ina kazi na wajibu wa uinjilishaji na umisionari. Rej. KKK 2205.

Liturujia Utatu Mtakatifu
29 Mei 2026, 16:02