Kard.Re:Hatuwezi kupata njia bora ya kumfikia Yesu bila kupitia Mama Yetu Maria
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Katika Siku ya Pili ya Mkutano Mkuu Maalum wa Makardinali Mjini Vatican uliotishwa na Baba Mtakatifu ambao ulianza Ijumaa tarehe 26 Juni kwa kufunguliwa naye kwa Misa Takatifu ili kujadiliana, kutafakari kwa kina na Makardinali kuhusu mantiki juu ya Kanisa la sasa na la Ulimwengu, Jumamosi tarehe 27 Juni 2026, Misa iliongozwa na Kardinali Giovanni Battista Re, Dekano wa Makardinali. Katika Misa iliyoadhimishwa kwa heshima ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa, asubuhi saa 1:30, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Dekano wa Makardinali katika mahubiri alikumbusha kwamba kwa njia ya Kristo, lakini pamoja naye na ndani yake, Mama Yetu yupo na anatenda katika Kanisa na duniani kwa ajili ya wokovu wa kila mwanamume na kila mwanamke. Na atusindikiza tunapokabiliana kwa busara na changamoto kubwa za wakati wetu, zinazojulikana kwa utamaduni wa nguvu na kutusaidia kujenga ustaarabu wa udugu, upendo, na amani.
Yesu alitupatia Zawadi ya Mama Yetu Maria
Tafakari ya Kardinali ilijikita kikamilifu kwenye kifungu cha Injili ya simulizi la Yohane, ambacho kilielekeza mawazo na moyo hadi Kalvari, wakati muhimu zaidi katika historia ya mwanadamu, ya sadaka ya ukombozi wa Kristo kwa ajili ya wokovu wetu. Ni wakati ambapo Yesu, msalabani, kabla ya kupumua pumzi yake ya mwisho, baada ya kujitoa katika Ekaristi katika Chumba cha Juu, cha Karamu Kuu, alitupatia zawadi nyingine isiyoelezeka ya Mama Yetu kama Mama."
Ubinadamu unahitaji msaada wa Mama
Kardinali alisema kuwa hiki, ni kifungu chenye maana ya kina, ambacho kinatuzungumzia kuhusu nafasi ya mama ya Maria katika maisha ya waamini wote. Kiukweli, kabla ya kumkabidhi Mama Yetu kwa Mtume Yohane, Yesu alimkabidhi Mama Yetu Yohane, na katika Yohane anatukabidhi sisi sote. Hasa zaidi, "Kristo alimkabidhi Mama Yetu umama wa kiroho wa ulimwengu wote unaoanzia Mtume Yohane hadi Wakristo wote katika karne zote, Kardinali Re alisisitiza, akiongeza kwamba wazo la kwanza la Kristo alipokufa msalabani halikuwa kwa ajili ya mama yake, ambaye tangu wakati huo alibaki peke yake, bali kwa ajili ya ubinadamu, ambao unahitaji msaada wa mama." Kwa hivyo, chini ya Msalaba, "Umama wa kiroho wa Mama Yetu unazaliwa ndani ya upeo wa ubinadamu wote; umama unaochochewa na hamu ya kutusaidia kukua kiroho na kwa kuzingatia mahitaji na mateso yote ya kila kiumbe cha mwanadamu, na daima anapatikana kutusaidia."
Chanzo cha ibada ya Maria ni Golgotha
Kardinali Re aidha alieleza kwamba chanzo cha ibada ya Maria ni Golgotha. "Tangu wakati huo, katika mabadiliko ya furaha na huzuni ya maisha, tunaweza kutegemea msaada wa mama, ambaye yuko karibu na Mungu, na kwa hivyo anaweza kutuombea, na yuko karibu nasi kwa upendo wa mama na hakuna shida na wasiwasi wetu unaomtoroka, Kardinali Re alibainisha. Mtakatifu Paulo VI alifafanua zaidi hili katika Waraka wake wa Kitume Marialis Cultus, akisema kwamba "Mungu alimweka Mama Yetu kwenye njia ya kila mwanamume na mwanamke, ili atulinde na kutuonesha njia." Yeye, ambaye pale Kalvari aliteseka kwa ajili yetu, ili tuweze kuwa na nguvu na ujasiri wa kukabiliana na majaribu mengi, yupo katika kila wakati muhimu katika historia ya wokovu.” Kardinali Re alihitimisha kuwa: “Maria yuko katikati ya fumbo la Umwilisho. Mungu, katika mipango yake ya ajabu, alichagua kuja kwetu katika Kristo, na hatuwezi kupata njia bora ya kumfikia kuliko kupitia Mama Yetu."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.