Sudan:Jumuiya ya kimataifa ichukue hatua kuzuia janga la EL Fasher &El Obeid
Habari za Umoja wa Mataifa
Tume huru ya Umoja wa Mataifa ya Kuchunguza Ukweli kuhusu mzozo unaoendelea Sudan ilitoa Ripoti yake tarehe 8 Julai 2026 huko Geneva Uswiss, ikibanisha kuwa mauaji ya halaiki, ubakaji wa makundi na utekaji wa kimfumo wa wanawake na wasichana unaodaiwa kufanywa na vikosi vya Msaada wa Haraka (RSF) mjini El Fasher vinaonesha viashiria vya uhalifu wa mauaji ya kimbari. Wakati huo huo, Tume hiyo ilitangaza uchunguzi wa dharura kuhusu madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu na sheria za kimataifa za kibinadamu mjini El Obeid, ambako kuna hofu ya kurudiwa kwa mtindo huo wa ukatili.
Jumuiya ya Kimataifa lazima izingatie haya na kuchukua hatua
Mwenyekiti wa Tume hiyo ya uchunguzi, Mohamed Chande Othman, alisema, "Mifumo tuliyoibaini El Fasher, ikiwemo kuzingirwa kwa mji, mashambulizi dhidi ya miundombinu ya kiraia, vizuizi vya misaada ya kibinadamu na ukiukwaji mkubwa dhidi ya raia, ni onyo kali. Jumuiya ya kimataifa lazima izingatie mafunzo haya na ichukue hatua kuzuia janga jingine." Tume hiyo ilieleza kuwa zaidi ya wakazi nusu milioni pamoja na zaidi ya watu 100,000 waliokimbia makazi yao wako hatarini El Obeid kutokana na mashambulizi na kuzorota kwa hali ya usalama.
Mjumbe mtaalamu Mona Rishmawi alisema, "Mafunzo ya El Fasher hayapaswi kupuuzwa... Jumuiya ya kimataifa bado ina nafasi ya kuzuia uhalifu mwingine mkubwa. El Obeid haipaswi kuwa eneo jingine la uhalifu. "Ripoti ilisisitiza umuhimu wa uwajibikaji kupitia ushirikiano na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), huku ikiendelea na uchunguzi wake na kuahidi kuwasilisha matokeo kwa Baraza la Haki za Binadamu na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.