Tafuta

Tafakari ya Neno la Mungu Dominika ya 26 ya Mwaka C wa Kanisa: Maskini wanayo nafasi ya pekee katika maisha na utume wa Kanisa. Tafakari ya Neno la Mungu Dominika ya 26 ya Mwaka C wa Kanisa: Maskini wanayo nafasi ya pekee katika maisha na utume wa Kanisa. 

Tafakari Neno la Mungu Dominika 26: Wajibu na Haki Jamii: Hukumu

Katika tafakari ya Liturujia ya Neno la Mungu Dominika ya ishirini na sita ya Kipindi cha Mwaka C, Kanisa linatuita kuwa wenye haki na kufanya kazi kwa ajili ya uzima wa milele. Kwa hiyo, linatutia hamasa tuweze kujitolea na kuwa watu wenye bidii katika “vita vyema vya imani hata kufunuliwa kwa Bwana.” Huduma kwa maskini na wanyonge ni sehemu ya upendo kwa watu wa Mungu.

Na Padre Efrem Msigala, OSA., - Dar Es Salaam.

Karibu mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican na msomaji wa Vatican News katika tafakari ya Liturujia ya Neno la Mungu Dominika ya ishirini na sita ya Kipindi cha Mwaka C, Kanisa linatuita kuwa wenye haki na kufanya kazi kwa ajili ya uzima wa milele. Kwa hiyo, linatutia moyo tuweze kujitolea na kuwa watu wenye bidii katika “vita vyema vya imani hata kufunuliwa kwa Bwana.” Masomo yote ya dominika hii ni mwendelezo wa masomo ya Dominika ya 25 ya Mwaka C wa Kanisa yakizingatia siku ya hukumu ya Mungu. Muhimu zaidi, yakielekeza kwenye mwisho wa wasio haki, ushindi na faraja ya maskini na waadilifu. Katika somo la kwanza, Nabii Amosi anaendeleza mafundisho yake dhidi ya matajiri na watu mashuhuri wa jamii wanaowadhulumu wanyonge na maskini. Anatangaza hukumu ya Mungu kwa wale wanaopata furaha na faraja kutokana na kugandamiza maskini na dhaifu. Amosi ni Nabii wa haki ya kijamii. Kupitia yeye, Mungu alilaani kila aina ya ukosefu wa haki miongoni mwa watu wa Israeli. (Am 6:1a, 4-7), Amosi alikemea maisha ya kupita kiasi na anasa ya watu, bila kujali mahitaji ya maskini katikati yao. Aliwatangazia hukumu ya Mungu, Anasema: “Kwa hiyo, sasa watakuwa wa kwanza kwenda utumwani, na karamu yao ya anasa itakomeshwa.”

Waamini wawe ni vyombo vya huruma na faraja kwa maskini duniani.
Waamini wawe ni vyombo vya huruma na faraja kwa maskini duniani.

Katika Barua yake ya kwanza kwa Timotheo (1Tim 6:11-16), Mtakatifu Paulo anamsihi awe kiongozi mzuri wa watu aliokabidhiwa:  Anasema: “Ufuate uadilifu, utauwa, imani, upendo, saburi na upole. Kwa kweli, himizo hili linatumika kwa kila mkristo. Hatuwezi kuridhika na kutojali matukio yanayotuzunguka, matukio ya kutojali haki  za watu na hasa wanyonge. Kwa hiyo, agizo la Mtume ni hili, anasema: “Nawaagiza … kushika amri pasipo mawaa wala lawama, hata kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo...! Injili ya leo ni ya kipekee kwa maana kwamba inagusa kipengele muhimu sana cha maisha yetu ya Kikristo na kuamini. Hiyo ni, “eskatolojia” au “taalimungu ya mambo ya nyakati.” Kwanza, inahusu mambo matatu muhimu sana ya mwisho: Kifo, hukumu, na thawabu mbinguni au kuzimu (Ebr 9:27). Pili, inatuhusu na hutuhakikishia faraja ya wale wanaoomboleza sasa duniani kama Kristo alivyoahidi: “Heri wenye huzuni maana hao watafarijiwa (Mt 5:4). Kustarehe kupindukia, na maonyesho ya utajiri hapa duniani ambayo hayatoi chanya katika maisha ya wengine hasa maskini, hayatatunufaisha sana mwisho wa nyakati. Hayatatuhakikishia tiketi yetu katika “kifua cha Ibrahimu.” Kwa hiyo, tunapaswa kuwa makini na neno la Mungu tunalosikia kila siku, linatuita kutumia mali yetu ya kidunia kuwasaidia maskini na wanyonge.

Kwa hivyo, kuzingatia ukweli kwamba ulimwengu huu utapita hutusaidia sana kujitayarisha kwa ufalme wa milele. Ni wale tu ambao wamekaza fikira na wasiokengeushwa na starehe nyingi za ulimwengu huu ndio watakaomwona kwa urahisi na kumhudumia Kristo katika “Lazaro” anayewazunguka. Hatimaye, kupitia somo la pili la Dominka hii, Paulo anatushauri hivi: “Kama wewe mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; fuata haki na piga vita vizuri vya imani...”  Hata hivyo, ni wale tu wanaoifanyia kazi kwa imani, subira, upendo, uungwana, uchaji kwa Mungu na kwa wengine ndio watafika hapo. Ni wale tu wanaoonyesha huruma kwa maskini, wanyonge, na wenye haki ndio wenye kukubaliwa kifuani mwa Ibrahimu. Huo ni, ufalme wa milele, ambapo “mambo bora zaidi yanaweza kutumainiwa.” Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican na Msomaji wa Vatican News.  Maandiko matakatifu ya injili ya leo yanatualika kwa mara nyingine tena kutafakari maana ya upendo na wema. Kuna yule tajiri asiyetajwa jina ambaye ana jirani yake masikini aitwaye Lazaro, mhitaji.  ‘Lazaro’ kihalisi maana yake, ‘Mungu husaidia’. Masikini anaonekana sana kwa sababu analala kwenye lango la tajiri.

Kuna aina mbalimbali za umaskini duniani: Hali, fedha, maadili na utu wema.
Kuna aina mbalimbali za umaskini duniani: Hali, fedha, maadili na utu wema.

Lazaro anatamani sana upendo wa jirani yake, lakini haupati. Anatamani kupata chakula toka kwa jirani yake anaishia kula makombo yaliyoanguka mezani pa tajiri. Hivyo anategemea tu upendo wa Mungu kwa kukosa wa jirani. Tajiri, licha ya utajiri wake, alifikiria vazi lake la zambarau, kitani safi, na karamu za kila siku (Lk 16:19) vingeweza kumpa furaha na ustawi. Mwishoni mwa hadithi, nafasi za wahusika zinabadilishwa, na ukweli unawekwa wazi. Katika mabadiliko ya matukio ya maisha kama kifo, tajiri ‘anazikwa’ tu, huku Lazaro akibebwa hadi kifuani mwa Ibrahimu. Tajiri anatengwa na karamu ya mbinguni. Anakuwa mwathirika wa shimo ambalo alikuwa ameunda kwa kutomjali kwake Lazaro maskini. Injili inahusu mtazamo wetu kwa Mungu, na mtazamo wetu kwa jirani zetu. Kwa hiyo injili inajibu swali letu kwanini nipende. injili yanatufundisha kwamba upendo na fadhili ni muhimu kwa ustawi wetu wa kudumu na furaha ya kweli. Wale wanaomtumaini Mungu kweli watafurahia ustawi, kwa sababu wataweza kuwa na huruma. Ingawa Yesu katika mahubiri yake alirudia Kanuni Bora iliyopendekezwa na Sheria na Manabii ( Mt 7:12; Lk 6:31 ) mwaliko wake wa upendo unategemea uzoefu wa upendo wa Mungu Mwenyewe. Katika Injili ya Lk 6:36, anasema, “Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma.” Kipimo cha kupimia upendo wangu kwa jirani sio tu upendo wangu kwangu mwenyewe, lakini ni upendo wa Mungu kwangu.

Na katika Injili ya Yohane, Yesu anafafanua zaidi (Yn 13:34; pia 15:12): “Nawapeni amri mpya: mpendane; kama vile mimi nilivyowapenda ninyi.” Yohana anaendelea kutoa ufafanuzi juu ya hili katika waraka wake wa kwanza: akisema “Rafiki zangu wapenzi, na tupendane, kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, na kila apendaye ni mtoto wa Mungu, naye anamjua Mungu…. Huu ndio ufunuo wa upendo wa Mungu kwetu, kwamba Mungu alimtuma Mwanawe pekee ulimwenguni ili tuwe na uzima kupitia yeye. Upendo uko katika hili: si sisi tuliompenda Mungu, bali Mungu alitupenda sisi hata akamtuma Mwanawe ili aondoe dhambi zetu. wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda sana, sisi pia tunapaswa kupendana. ( 1Yoh 4:7-11 ). Maisha ya Kikristo yamo katika kumfuata Yesu kikamilifu. Hakuna nafasi ya kuridhika, uvivu na uzembe. Tunapaswa kukataa kila aina ya ukosefu wa haki na ukosefu wa adili, ambao nabii Amosi alilaani vikali. Kwa njia nzuri zaidi, twapaswa kutii himizo la Mtakatifu Paulo la “kufuatia uadilifu, utauwa, imani, upendo, saburi na upole.” Mungu alituumba kama watoto wake katika uhuru. Anataka tuwe huru kutokana na utumwa wowote wa dhambi na mambo ya kidunia. Ndiyo sababu, katika mengi ya mafundisho yake, Yesu alisisitiza juu ya kujitenga na kujinyima: “kauze ulivyo navyo unifuate.”

Waamini wawe ni vyombo vya huruma, upendo na faraja kwa maskini.
Waamini wawe ni vyombo vya huruma, upendo na faraja kwa maskini.

Kijana tajiri alitaka kupata uzima wa milele, lakini hakuweza kuupata kwa sababu hakuwa huru wala hakuweza kuacha mali yake. Tajiri katika Injili dominika hii hangeweza kuacha mali yake pia. Na katika utumwa wake wa starehe ya kimwili na anasa, alipofushwa nao na akachagua kumwacha Lazaro malangoni mwake. Hakuwa huru. Lakini utumwa wa vitu vya kimwili unaweza kutokea si kwa matajiri tu, bali pia kwa maskini. Kuna watu wengi maskini ambao wamejishughulisha sana na kutafuta mlo wao ujao na kwamba hawana muda zaidi wa kumfikiria Mungu. Wao pia ni watumwa wa vitu vya kimwili. Ndio maana inatubidi kila mara tujichunguze, mahangaiko yetu Mungu anapewa nafasi? Na je tunawatendea nini wale ambao ni wahitahitaji?

Dominika 26 Mwaka C wa Kanisa.
23 September 2022, 15:38