Tafakari Dominika ya Kwanza Kwaresima: Vishawishi na Majaribu
Na Padre Paschal Ighondo, - Vatican.
Tafakari ya Neno la Mungu, dominika ya Kwanza ya Kipindi cha Kwaresima mwaka A wa Kiliturujia katika Kanisa. Kipindi cha Kwaresima kwa mwaka huu 2026 kinanogeshwa na ujumbe wa Baba Mtakatifu Leo XIV kwa kauli mbiu: “Kusikiliza na kufunga: Kwaresima kama Kipindi cha Wongofu wa ndani.” Kwaresima ni kipindi ambacho Kanisa kama Mama na Mwalimu, anawaalika watoto wake kutoa kipaumbele cha pekee kwa Fumbo la Mungu katikati ya maisha yao, ili imani ipate tena nguvu na mioyo ya waamini isipotee katikati ya mahangaiko na bughudha za maisha ya kila siku. Kila safari ya wongofu wa ndani huanza pale waamini wanaporuhusu Neno la Mungu liwafikie na kulikaribisha kwa moyo wa unyenyekevu. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema, kuna uhusiano kati ya karama ya Neno la Mungu, Nafasi ya Ukarimu na mabadiliko ambayo Neno hili linaleta. Kwa sababu hiyo, safari ya Kwaresima inakuwa ni fursa muafaka ya kusikiliza sauti ya Mungu na hivyo kupyaisha tena maamuzi ya kumfuasa Kristo Yesu, kwa kutembea katika njia ile iendayo Yerusalemu ambako Fumbo la Pasaka yaani: Mateso, kifo na ufufuko vinapata utimilifu wake. Ujumbe mkuu umejikita katika majaribu na namna ya kupambana nayo kwa kuwa na Muunganiko na Mungu Baba aliye asili ya utakatifu na wema wote, kwa njia ya sala, kufunga na kufanya toba ya kweli. Tukifanya hivyo, Yeye katika maneno ya wimbo wa mwanzo anatuahidi kuwa nasi na kutuokoa akisema; “Ataniita nami nitamwitikia; nitamwokoa na kumtukuza; kwa siku nyingi nitamshibisha” (Zab. 91:15-16). Ni katika tumaini hili mama Kanisa katika sala ya mwanzo anasali hivi; “Ee Mungu Mwenyezi, utujalie tuzidi kuifahamu siri ya Kristo na kupata manufaa yake katika mwenendo wetu mwema kwa mfungo wa Kwaresima wa kila mwaka.” Nao Mababa Askofu wa Kanisa Katoliki Tanzania katika ujumbe wa Kwaresima 2026, wanatuasa tumwombe Mungu azitie moyo roho zetu na nia zetu hata tunapokutana na vikwazo vya namna mbalimbali tusichoke kutenda mema, tukitambua kuwa kutenda mema ni safari ambayo inapaswa kukua siku kwa siku kwa nguvu zake Mungu.
Somo la kwanza ni kutoka katika Kitabu cha mwanzo (Mwa 2:7-9, 3:1-7). Nalo limegawanyika katika sehemu kuu mbili. Sehemu ya kwanza inatueleza kuwa asili na uzuri wa mwanadamu na vitu vyote vilivyomo, vinavyoonekana na visivyooneka, ni Mungu aliyemuumba mtu mzima mwili na roho, akampa maisha ya heri na amani bila kufa. Hali hii ingedumu tu iwapo mtu angetii enzi na mamlaka ya Mungu. Katekisimu ya Kanisa Katoliki ikinukuu maandiko matakatifu inatufundisha hivi; “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanaume na mwanamke aliwaumba. Hivyo mtu ana nafasi ya pekee ndani ya uumbaji: ni sura ya Mungu; katika asili yake anaunganisha ulimwengu wa kiroho na wa vitu; amemwumba mume na mke; amemfanya rafiki yake. Hivyo kati ya viumbe vyote vinavyoonekana, mtu peke yake ana uwezo wa kumfahamu na kumpenda Muumba wake. Ni yeye kiumbe peke yake juu ya nchi ambacho Mungu alikikusudia kwa ajili yake mwenyewe. Yeye peke yake ameitwa kushiriki uzima wa Mungu kwa akili na upendo. Ameumbwa kwa ajili hiyo na ndiyo sababu ya msingi wa heshima yake” (KKK 355-356). Sehemu ya pili ya Somo hili inaeleza matokeo ya mwanadamu kukengeuka, kuasi, kutokutii enzi na mamlaka ya Mungu, kukaidi amri na maagizo yake, kujiamulia lipi liwe jema na lipi liwe baya, kuchukua nafasi ya Mungu, kutaka kuwa kama Mungu, kuamua kipi kiwe kibaya na kipi kiwe chema. Hali hii inaitwa anguko la kwanza la mwanadamu, kwa ushawishi wa nyoka, ishara ya ibilisi, mshawishi na mjaribu mkuu, chanzo cha dhambi, mateso, mahangaiko, na kifo kuingia ulimwenguni. Hali hii ilimfanya mwanadamu kujiona yuko uchi, kuwa dhaifu, kutojiweza, kukosa furaha, na amani ndani mwake kwa kujitenga na kuwa mbali na Mungu, hivyo kuamua kujificha.
Amani ambayo aliyokuwa nayo kwa haki ya asili ilivunjika, na utawala wa roho juu ya mwili uliotokana na vipawa vya kiroho, uliharibika. Umoja kati ya mwanaume na mwanamke ukawa wa wasi wasi, mahusiano yao yakajeruhiwa na tamaa na kuwa na hali ya kutawaliwa. Amani na viumbe vingine ikavunjika, kukawa na uadui. Hivyo mauti ikaingia katika historia ya mwanadamu (rej. KKK 396-400). Kipindi cha Kwaresima ni kuomba huruma ya Mungu, kujipatanisha naye, Yeye aliye asili ya wema wote, ili aturudishie hadhi tuliyoipoteza. Ni katika mukatadha huu zaburi ya wimbo wa katikati inasema hivi; “Uturehemu, ee Bwana, kwa kuwa tumetenda dhambi. Ee Mungu, unirehemu, sawa sawa na fadhili zako, kiasi cha wingi wa rehema zako, uyafute makosa yangu. Unioshe kabisa na uovu wangu, unitakase dhambi zangu. Maana nimejua mimi makosa yangu, na dhambi yangu i mbele yangu daima. Nimekutenda dhambi Wewe peke yako. Na kufanya maovu mbele za macho yako. Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu. Usinitenge na uso wako, wala roho yako mtakatifu usiniondolee. Unirudishie furaha ya wokovu wako; unitegemeze kwa roho ya wepesi. Ee Bwana, uifumbue midomo yangu, na kinywa changu kitazinena sifa zako” (Zab. 51 : 1-4, 10-12, 15).
Somo la pili ni kutoka katika Waraka wa Mtume Paulo kwa Warumi (Rum 5:12-19). Ujumbe wake ni kuwa Mungu katika hekima yake na upendo wake aliugeuza ubaya wa mwanadamu kuwa wema na akaibadili laana kuwa baraka ya thamani kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wa mwanae Yesu Kristo. Dhambi na mauti vilivyoingia duniani kwa njia ya Adamu wa kwanza, madhara yake yametokomezwa kwa njia ya Adamu wa pili, Bwana wetu Yesu Kristo, kwa neema yake inayoshinda dhambi na mauti. Hii ndiyo siri kuu ambayo mama Kanisa anaikiri katika sala ya mwanzo anapotuombea akisali hivi; “Ee Mungu Mwenyezi, utujalie tuzidi kuifahamu siri ya Kristo na kupata manufaa yake katika mwenendo wetu mwema kwa mfungo wa Kwaresima wa kila mwaka”. Injili ni ilivyoandikwa na Mathayo (Mt 4:1-11). Ni simulizi la kujaribiwa kwa Yesu na shetani, baada ya ubatizo wake, akiwa Jangwani akifunga na kusali kwa mda wa siku 40, hata akaona njaa. Katika mazingira na hali hiyo, shetani alimjaribu na kumshawishi ili achague uzuri wa dunia hii, asitukomboe, tubaki katika utawa wake. Lakini Yeye akimtumaini Mungu Baba aliyashinda majaribu yote ya Shetani. Kwaresima kwetu ni kipindi cha kupambana na majaribu ya shetani kwa silaha za sala, mafungo na toba ya kweli, tukifuta mfano wake Kristo kama utangulizi wa dominika hii unavyotuelekeza ukisema; “Yeye alifunga chakula siku arobaini, akaonyesha ubora wa namna hiyo ya kufanya kitubio. Amewaepusha watu wote na hila za nyoka wa kale, na kutufundisha kushinda chachu ya uovu.”
Majaribu ya Yesu ni kielelezo cha majaribu yetu tunayokutana nayo katika maisha yetu kama vile; kutafuta miujiza kwa kila hitaji letu la kimwili, kutafuta ukuu, utawala, mamlaka, na ufahari kwa kila njia, ikiwa ni pamoja na kuwatendea wengine mabaya, hata kuwaua na kumwabudu shetani. Kristo Yesu alizikataa ahadi za shetani, kwa nguvu ya sala, kufunga na kuweka tumaini lake lote kwa Mungu Baba, akamshinda shetani na hila zake zote. Kipindi hiki cha Kwaresima tufunge na kusali, tukiombeana na kutendeana mema ili tuweze kumshinda shetani na hila zake kama Mababa Askofu katika ujumbe wa Kwaresima 2026, wanavyotuasa wakisema; “Wewe mtu wa imani, wategemee waamini wenzako kwa ajili ya kutiwa moyo na kuwajibika, ukitambua kwamba safari ya imani ni bora zaidi katika kutembea pamoja. Zingatia kwa makini ushiriki wako katika Jumuiya Ndogondogo za Kikristo, Vyama vya Kitume; wajibu wako wa uongozi ndani ya familia, Kanisa, kwenye jamii, na mahali pengine popote unapokabidhiwa majukumu. Ndani yake sehemu hizo, utapata usaidizi wa kukutia moyo pale unapoelekea kukata tamaa”. Kwa pamoja na moyo mmoja, tusali na tufunge kwa ajili ya dhambi za mauaji ya kinyama ya ndugu zetu kwa ajili ya kulinda maslahi na mamlaka yetu. Tusali na kufunga kwa ajili ya wanaotafuta mali kwa njia zisizo halali, tulie na kuomboleza, ili waweze kumrudia Mungu pamoja nasi. Kwa kuwa kiongozi wetu Kristo aliyashinda yote kwa kumtumainia Mungu. Nasi tukimtegemea tutashinda. Lakini lazima tujikite katika kufunga, kutendeana mema bila kuchoka, kusali sala binafsi, kushiriki Misa Takatifu na kupokea sakramenti, hasa Kitubio na Ekaristi Takatifu. Ni katika tumaini hili mama Kanisa katika sala baada ya komunyo anatuombea akisali hivi; “Ee Bwana, sisi tumekula mkate wa mbinguni unaolisha imani, unaoleta tumaini, na kuzidisha mapendo. Tunakuomba utuwezeshe kumtamani Yeye aliye mkate hai wa kweli, tuweze kuishi kwa kila neno litokalo katika kinywa chako”. Na hili ndilo tumaini letu. Tumsifu Yesu Kristo!