Tafuta

Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni: Mtakuwa ni Mashuhuda wangu hadi miisho ya dunia. Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni: Mtakuwa ni Mashuhuda wangu hadi miisho ya dunia.   (Vatican Media)

Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni: Siku ya 60 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni 2026

Ni katika muktadha wa maadhimisho ya Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni sanjari na Maadhimisho ya Siku ya 60 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni yanayonogeshwa na kauli mbiu “Kuhifadhi Sauti na Nyuso za Binadamu.” Papa Leo XIV anawataka wadau wa tasnia ya mawasiliano kuhakikisha kwamba, uvumbuzi wa teknolojia, hasa matumizi ya teknolojia ya akili unde, inamhudumia binadamu badala ya kuchukua nafasi au kupunguza utu, heshima na haki msingi!

Na Padre Octavian O. Hinju, CP-JUCo, Morogoro (Tz).

Katika kipindi cha siku arobaini Kristo Yesu mfufuka aliwatokea wanafunzi wake akiwapa katekesi ya kina kusuhu Fumbo la Pasaka yaani: Mateso, kifo na ufufuko wake kadiri ya mpango wa Mungu. Mama Kanisa anasadiki na kufundisha kwamba, Kristo Yesu baada ya kusema nao, akachukuliwa mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. Mwili wa Kristo ulitukuzwa wakati ule ule alipofufuka kama zinavyoshuhudia hali mpya na za kimungu ambazo tokea hapo umebaki nazo daima. Lakini kile kipindi cha siku arobaini ambako alizoea kula na kunywa pamoja na wafuasi wake, na kuwafundisha juu ya Ufalme wa mbinguni, utukufu wake bado ulifunikwa na alama za ubinadamu wa kawaida. Tokeo la mwisho la Yesu linakamilika na kuingia bila kurudi kwa ubinadamu wake katika utukufu wa Mungu uliojionesha katika sura ya wingu na mbingu (Lk 24:51) ambako tangu hapo ameketi kuume kwa Mungu. Kwa namna moja tofauti kabisa na ya pekee atajionesha kwa Paulo “kama mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake” katika tokeo la mwisho lililomfanya kuwa Mtume. Hali iliyofunikwa ya utukufu wa Kristo Mfufuka kipindi hiki inaonekana katika maneno yake ya fumbo kwa Mariamu Magdalena: “Sijapata kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, ninapaa kwenda kwa Baba yangu, naye ni Baba yenu.” Yn 20:17 Hii inaonesha tofauti ya kujidhihirisha kati ya utukufu wa Kristo Mfufuka na ule wa Kristo aliyetukuzwa kuume kwa Baba. Tukio ambalo kwa upande mmoja ni la kihistoria na bora sana linaloonesha kupita toka upande mmoja kwenda upande mwingine. Lakini yote yanabaki yakiwa yameungana kabisa na lile la kwanza yaani kushuka kutoka mbinguni kulikotekelezwa katika Fumbo la Umwilisho. Ubinadamu ukiachiwa katika nguvu zake za maumbile hauwezi kufika kwenye nyumba ya Baba wa milele. Kristo Yesu peke yake ameweza kumfungulia mwanadamu njia hii “ili tukae tukiamini kwamba sisi tulio viungo vyake ametutangulia huko aliko Yeye aliye kichwa chetu na shina letu na kwamba, akiisha inuliwa juu ya nchi atawavuta wote kwake.” Huku ni kuinuliwa juu ya Msalaba ambako huonesha na kutangaza kuinuliwa kwa kupaa mbinguni. Huo ndio mwanzo wake.

Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni: Kutukuzwa kwa ubinadamu wetu
Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni: Kutukuzwa kwa ubinadamu wetu

Mbinguni Kristo Yesu anatekeleza Ukuhani wake daima, Yeye ni kiini na mtendaji mkuu wa Liturujia inayomheshimu Baba wa mbinguni. Kristo Yesu ameketi kuume kwa Baba, maana yake: ameketi katika utukufu na heshima ya Kimungu, ambaye Yeye aliyekuwako kama Mwana wa Mungu kabla ya nyakati zote, kama Mungu, na mwenye uwamo mmoja na Baba, anaketi kimwili, baada ya kumwilishwa na baada ya mwili wake kutukuzwa. Kuanzia hapo Mitume wamekuwa ni mashuhuda wa Ufalme usiokuwa na mwisho. Rej. KKK 659-664. Ni katika muktadha wa maadhimisho ya Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni, Dominika tarehe 17 Mei 2026, sanjari na Maadhimisho ya Siku ya 60 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni yanayonogeshwa na kauli mbiu “Kuhifadhi Sauti na Nyuso za Binadamu.” Baba Mtakatifu Leo XIV anawataka wadau wa tasnia ya mawasiliano ya jamii kuhakikisha kwamba, uvumbuzi wa teknolojia, hasa matumizi ya teknolojia ya akili unde, inamhudumia binadamu badala ya kuchukua nafasi au kupunguza utu, heshima na haki msingi za binadamu. Fumbo la Pasaka ndilo Fumbo kuu linalobeba Imani yetu. Yesu anapopaa mbinguni, hatuachi peke yetu bali anatukabidhi kazi ya uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili ndio maana aliwaambia Mitume walipomuuliza kuhusu wakati wa kurudisha ufalme: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi” (Mdo 1:7-8.) Huu ni wito kwetu kuwa mashuhuda wa imani, matumaini na mapendo kwake kupitia matendo na maisha yetu ya kila siku hapa duniani.

Baada ya Siku 40 za mateso, kifo na ufufuko wake Kristo Yesu anapaa mbinguni.
Baada ya Siku 40 za mateso, kifo na ufufuko wake Kristo Yesu anapaa mbinguni.

Sherehe ya Kupaa kwa Bwana Mbinguni huadhimishwa siku ya 40 baada ya Pasaka. Ni sherehe inayotukumbusha Yesu Kristo kupaa mbinguni na kuketi mkono wa kuume wa Baba, akituahidia Roho Mtakatifu na kututuma kuwa mashahidi wake ulimwenguni kote. Itakumbukwa kuwa, kwa Fumbo la Umwilisho Mungu alichukua hali ya kibinadamu katika Nafsi ya pili, akazaliwa na Bikira Maria, akakaa na kukua katika familia. Baada ya ubatizo wake akiwa na umri wa miaka 33 akaanza kazi ya kutangaza habari njema ya wokovu kwa muda wa miaka 3. Baadaye alikamata, akateswa, akasulibiwa na kufa kifo cha Msalaba. Baada ya siku tatu alifufuka na kurudia hali yake ya Kimungu na kupaa mbinguni mwili na roho. Hili ni tukio la kweli linalo sheheni uzito wa kihistoria linalo jidhihirisha wazi kama ishara ya kilele cha ukombozi wa mwanadamu. Kupaa kwa Bwana ni ukumbusho wa Fumbo la Yesu Kristo kupaa katika utukufu wa mbinguni akiwa na mwili wake mzima ambao Ijumaa kuu ulisulubiwa kwa mateso makali hata akafa, akazikwa na kufufuka siku ya tatu kadiri ya mapokeo na mafundisho tanzu yahusuyo Imani yetu. Ni kwamba imani yetu inafundisha ukweli kuwa siku 40 baada ya kufufuka, Yesu alipaa mbinguni mbele ya wanafunzi wake. Ni Dhahiri kwamba Kristo hataonekana tena katika hali ya mwili wa kibinadamu mpaka atakapo rudi siku ya mwisho.

Mtakuwa Mashuhuda wangu hadi miisho ya dunia
Mtakuwa Mashuhuda wangu hadi miisho ya dunia   (@Vatican Media)

Mpendwa Msomaji na Msikilizaji wa Vatican News, katika Maandiko Matakatifu kuna nukuu nyingine nyingi zinazodhihirisha kuwa Kristo baada ya ufufuko wake alipaa mbinguni na ameketi mkono wa kuume wa Mungu akituombea. Hebu tusome baadhi ya nukuu hizi; “Kristo Yesu ndiye aliyekufa, naam, zaidi ya hayo, ndiye aliyefufuka kutoka kwa wafu, yuko mkono wa kuume wa Mungu, naye ndiye anayetuombea” (Rom. 8:34). “Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni” (Mdo 1:11). “Mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu” (Kol 3:1). Jamii ya wakristo inahusishwa na tukio la kupaa kwake, kwa sababu yeye ni kichwa chao, na wao ni viungo vya mwili wake yaani kanisa: hivyo amewatangulia kwa Baba awaombee Roho Mtakatifu ili siku moja wafike kwake mbinguni. Ni katika ukweli huu Yeye mwenyewe alihidi akisema hivi “Mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi muwepo” (Yn. 14:3). Yesu alisema, “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu… Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu” (Yn. 18:36,37).

Waamini wanaitwa na kutumwa kutangaza Injili ya Kristo
Waamini wanaitwa na kutumwa kutangaza Injili ya Kristo   (@Vatican Media)

Mpendwa Msomaji na Msikilizaji wa Vatican News, Mababa wa Kanisa wanalitazama tukio hili la kupaa kwa Bwana sio tu kama tukio la kihistoria ya kwamba Kristo alipaa mbinguni bali kama furaha ya ushindi wa Kristo dhidi ya dhambi na mauti. Walifundisha kwamba Yesu alipaa katika hali ya kimwili ili kuunganisha hali yake ya ubinadamu na ile ya Utatu Mtakatifu. Na kwa kufanya hivyo mbingu zilifunguka, ubinadamu ukaunganishwa na umungu na hivyo kuandaa njia ya wanadamu kwenda kwa Baba wa milele. Mababa wa Kanisa wanaendelea kufundisha wakisisitiza kuwa; kwa tendo la kupaa kwake mbinguni ubinadamu wake Kristo ulitukuzwa. Ya kwamba kwa kupaa kwake mbinguni Kristo Yesu hakuutelekeza ubinadamu alioupokea angali hapa duniani “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli” (Yn. 1:14; badala yake aliusogeza karibu zaidi na uwepo wa Mungu; ndio maana Mt. Athanasi alisema hivi “Neno alifanyika mwili ili ubinadamu wetu uweze kutukuzwa.” Naye Mt. Gregori wa Nyssa alisema kwamba “tukio la kupaa Bwana ni tendo la juu zaidi ambalo linaonesha kuwa ubinadamu unaweza kukaa pamoja na umungu.” Ni tukio linaloonyesha kuwa muungano na utimilifu wetu ni Kristu, “Mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi muwepo” (Yn. 14:3). Mt. Augustino wa Hippo Askofu na Mwalimu wa Kanisa alifundisha hivi, ‘kwa kuwa kimwili Kristu yuko mbinguni, basi anaungana nasi hapa duniani kwa njia ya neema yake na uwepo wake angavu, endelevu na wakudumu kwani katika Sakaramenti ya Ekaristi Takatifu tayari kiroho tuko pamoja naye katika makao ya milele mbinguni. Hili lilikuwa ni tukio la hakika la kutuandaa sisi juu ya ujio wa Roho Mtakatifu.

Fumbo la Pasaka ni Kiini cha Imani ya Kanisa
Fumbo la Pasaka ni Kiini cha Imani ya Kanisa   (@Vatican Media)

Somo la kwanza ni kutoka katika Kitabu cha Matendo ya Mitume (Mdo. 1:1-11). Katika somo hili Luka Mwinjili ambaye aliandika pia kitabu hiki cha matendo ya Mitume, anatusimulia wosia alio utoa Yesu kwa Mitume kabla hajapaa kwenda mbinguni kwa Baba yake. Kristu Yesu aliwataka Mitume kupeleka Habari zake duniani kote hata atakapo kuja tena, “basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu (Mt. 28:19). Baada ya maagizo haya Yesu “alichukuliwa juu na wingu likampokea wasimwone tena katika upeo wa macho lakini akawa pamoja nao kwa njia ya Roho Mtakatifu akiwaimarisha katika kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Nasi kwa njia ya ubatizo na kipaimara tumempokea Roho Mtakatifu hivyo hatuna budi kuwa mashahidi wa Imani yetu kwa Kristo katika maisha yetu ya kila siku. Kama waamini wabatizwa, wito na utume wetu tukiongozwa na Roho Mtakatifu si kujisema sisi wenyewe ya kuwa ni akina nani bali ni kumsemea na kumtangaza Yule aliyefufuka ili wamjue “na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yoh.17:3).

Atakaponyanyuliwa juu ya Msalaba atawavuta wote kwake
Atakaponyanyuliwa juu ya Msalaba atawavuta wote kwake

Mpendwa Msomaji na Msikilizaji wa Vatican News, somo la pili ni kutoka katika Waraka wa Mtume Paulo kwa Waefeso (Ef. 1:17-23). Somo hili ni sala ya Mitume inayotupa fundisho juu ya uweza na utajiri wa Mungu uliofunuliwa katika Yesu Kristo. Katika sala hii Paulo Mtume anasali akisema hivi “Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwisho wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo; na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.” Kumbe Kristo Mfufuka ndiye mshindi dhidi ya dhambi na mauti. Nasi tukiamini katika yeye basi hatuna haja ya kuwa na hofu, mashaka wala wasiwasi. Yeye ni Bwana na Mfalme wa mbingu na nchi nasi tuweke tumaini letu kwake ili tuokoke.

Mtakuwa Mashuhuda wa Injili hadi miisho ya dunia
Mtakuwa Mashuhuda wa Injili hadi miisho ya dunia   (@Vatican Media)

Injili ni kama ilivyoandikwa na Mathayo (Mt. 28:16-20). Leo tunasoma aya za mwisho za Injili ya Mathayo ambapo tunasimuliwa juu ya tokeo la mwisho la Yesu kwa wanafunzi wake katika mazingira ya kipasaka huko Galilaya. Mwinjili Mathayo anaweka wazi mambo makuu matatu ambayo yanatoa tafsiri mpya ya maisha na utume ndani ya Kanisa; mosi ni uwepo wa daima wa Mungu kati yetu, pili, utume wa kimisionari na tatu ni ahadi ya uwepo wa mfariji ndiye Roho Mtakatifu, Roho wa ukweli na Hekima. Kadhalika katika muhtasari wa sehemu hii ya Injili, tunaoneshwa nguvu na mamlaka ya Yesu juu ya mbingu na nchi; kama anavyosema Nabii “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani” (Danieli 7:14). Ni katika mamlaka hayo ya Kristu ana liachia kanisa chini ya uongozi wa Mitume jukumu kubwa la kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wake kwa njia ya ubatizo; utume endelevu na wakudumu “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu”. Katika usia wake Kristu anawataka Mitume kuwapa katekesi kuhusu yote aliyowaagiza; yaani “kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi”. Na kuwa yeye mwenyewe Yesu atakuwa na kanisa katika hali zote; “Na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.”

Kristo Yesu amepaa mbinguni kwa kelele za shangwe alleluiya
Kristo Yesu amepaa mbinguni kwa kelele za shangwe alleluiya

Mpendwa Msomaji na Msikilizaji wa Vatican News, Kumbe, kupaa kwake mbinguni hakumfanyi asiwepo nasi. Kristo Yesu yupo daima nasi ili kutuchunga na pengine swali la msingi tunaloweza kujiuliza hapa ni kuwa tuna maanisha nini tunaposema Yesu amepaa mbinguni? Itakumbukwa kuwa Wayahudi waligawa ulimwengu katika ngazi tatu. Anga kama mahali anapoishi Mungu. Dunia mahali ambapo viumbe vyote na binadamu wanapoishi na kuzimu kama mahali ambapo wafu wanaishi, pia mahali pa shetani. Mtazamo huu anao binadamu wa nyakati zote na mahali popote hata sasa. Lakini Mama Kanisa anatufundisha kuwa mbingu siyo mahali fulani juu bali ni hali ya utukufu. Ndiyo maana katika tukio la kugeuka sura kwa Yesu, Petro aliposhuhudia japo kidogo tu utukufu wa Yesu, alifurahi sana na kusema; “Bwana ni vizuri sisi kuwa hapa (Mt. 17:4). Mtume Petro alitamani ile hali ya utukufu iendelee kua nao. Kwa hiyo tunaposema ya kuwa Kristo amepaa mbinguni hatumaanishi kwamba ameenda mahali pa juu, bali ameingia katika hali ya Utukufu wa Mungu. Na hali hii ilitokea mara tu baada ya kufufuka kwake ndiyo maana aliweza kuingia katika chumba walichokuwepo mitume ijapokuwa milango ilikuwa imefungwa kwa kuwa alikuwa tayari katika hali ya utukufu. Kitendo cha kupaa kwenda juu ni suala tu la kutamadunisha namna yetu ya kufikiri na kuona mambo. Tunapo endelea kutafakari hayo ya kimungu tumwombe Kristu atutumie tena na tena hiyo zawadi ya Roho Mtakatifu ili tuweze kutimiza vema nyajibu zetu kwa Mungu na Kanisa. Tumsifu Yesu Kristo. 

Kupapa Bwana 2026
16 Mei 2026, 11:30