Ask.Mkuu Amani:Wito ni zawadi ya Imani na Ujasiri
Na Sr Ernestina Patrikck Lasway,SCA - Arusha,Tanzania.
Wito wa Upadre unaongozwa na Imani na Upendo, sawa na miito mingine ilivyo. Askofu Mkuu Isaac Amani alibainisha hayo, katika adhimisho la Misa Takatifu ya upadrisho iliyofanyika tarehe 9 Julai 2026 katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Theresia wa Mtoto Yesu Jimboni Arusha nchini Tanzania. Katika homilia yake, Askofu Amani alibainisha kuwa wito wa upadre unalenga kuwaongoza wengine kwa Mungu kama mchungaji afanyavyo kuwaongoza katika malisho yaliyo sahihi na salama.
Wajibu wa Padre katika Kanisa
Akiendelea na homilia yake, Askofu aliwaalika mapadre kuwalisha kondoo kwa maarifa na busara, kwa fahamu na usahihi. “Mapadre wanalo jukumu la kuwaongoza watu katika kumfuata Mungu kwa uchaji, kwa kufanya kazi na kuwaongoza katika toba ya kweli,” alikazia. Kwa kuongozwa na mfano wa Nabii Yeremia (Yer.23:4), anatuongoza kutupatia wachungaji ambao hawataleta hofu miongoni mwa watu na hilo ndilo kusudi la Mungu. Mapadre ni sawasawa na manabii, makuhani na wafalme, wanatengwa kwa kupakwa mafuta ili kumtolea Mungu sadaka na kumpatanisha mwanadamu na muumba wake. Katika historia ya wokovu, Mungu aliwatuma manabii kwa nyakati tofauti kuwaongoza watu katika utumishi adimilifu na kufanya Ibada adilifu,” alisisitiza.
Umuhimu wa kuwatii manabii
Manabii na mitume waliposikilizwa na watu,walipokea baraka, walipoenda kinyume na ujumbe wa manabii na mitume, waliadhibiwa. Katika Injili ya siku (Yh. 10:11-21) Yesu anajitambulisha kama Mchungaji Mwema. Mchungaji mwenye kuwaongoza kondoo katika malisho yaliyo salama. Walio wake wanamfuata katika njia sahihi na salama. Kumfuata mcunhuja sahihi kama Kristo alivyofanya Kristo kwa kumfuata Baba na kwa njia hii kumkomboa mwanadamu “Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya Kondoo zangu.”
Yesu Kristo Mchungaji Mkuu
“Mungu anamthibisha Bwana wetu Yesu Kristo kama Mchungaji mkuu. Kwa upendo wake kwa Mwanadamu, anaudhihirisha kwa njia ya Kristo. Kwa njia hii anawaita wengine kuwa wachungaji, walimu, manabii ili kuujenga mwili wa Kristo kwa majitoleo katika nafasi mbalimbali,” alibainisha Askofu Mkuu Amani. Kwa njia hii padre analo jukumu la kujifunza kila mara kutoka kwa mchungaji mkuu Yesu Kristo kwa ufanisi katika utume wa kila siku.
Umuhimu wa kusoma alama za nyakati
“Ili kuwa mchungaji mwema,” Askofu Mkuu Amani aliwataka mapadre wapya “kusoma vyema alama za nyakati. Kwa kuwa upadre ni kujitoa sadaka, mapadre wanapaswa kuwa tayari kujisadaka kwa ajili ya mambo yamhusuyo Mungu (Ebr. 5:1-14).” Katika utume wa kikuhani, mapadre wanapaswa kufanya kazi kwa ajili ya ufalme wa Mungu kwa kuwatumilkia watu wa Mungu katika hali zote. Kwa njia hii lazima padre kutumia katika utume na kuwahudumia watu wa Mungu kwa upendo na majitolea ya dhati.
Wanaitwa na Kutumwa
Mapadre wapya, mara baada ya upadrisho, walitumwa kufanya utume sehemu mbalimbali ndani na nje ya Tanzania. Miongoni mwao ni mapadre watatu wa Shirika la Wafransiskani Wakapuchini(OFMcap) na Kumi na moja wa Jimbo Kuu Katokili Arusha.
Mapadre hawa ni:
Padre Aplhonse Bahati, wa Parokia ya Mashati Rombo
Padre Epiphany Joseph Mushi wa Uru Shimbwe,
Padre Juvenalis Donasian Mwendapole wa Parokia ya Mt.Fransisco wa Assisi- Kwangulelo,
Padre Joseph Kweyemamu wa Parokia ya Mtakatifu Theresa Arusha,
Padre Vedastus Method Waziri wa Mkuu Rombo na Parokia ya Roho Mtakatifu Ngarenaro,
Padre Emmanuel Lazaro Mollel wa Parokia ya Polisingisi,
Padre Joseph Josephat wa Parokia ya Mtakatifu Ambrosi Kibuka – Sinoni,
Padre Emmanuel Mazoya Peter wa Parokia ya Maji ya Chai,
Padre Gido Adolfu Kimario wa Parokia ya Mtakatifu Karoli Lwanga- Usa River,
Padre Priva Julian Kirango kutoka Parokia ya Kristo Mfalme Chekereni,
Padre Erasto Otto Lekule wa Parokia ya Mtakatifu Simon Mtume Loruvani,
Padre Elton Njau wa Parokia ya Mtakatifu Yoseph Mume wa Bikira Maria- Patandi,
Padre Joseph Salvatory Chuwa OFMCap, Padre Adelardi Shirima OFMCap, na
Padre Jackson Noel Swai, OFMCap.
Tuwaombee mapadre wapya ili wadumu katika wito wao.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.