Padre wa Venezuela:Baadhi ya maeneo yasiyotambulika baada ya tetemeko la ardhi
Na Johan Pacheco – Vatican.
Kiwango cha maafa ni kikubwa sana. Eneo la La Guaira ndilo lililoharibiwa zaidi nchini kote. Baadhi ya maeneo hayatambuliki kwa sababu kila kitu kimeharibiwa na kuenea maeneo ambayo huenda yakalazimika kuhamishwa na kutelekezwa. Alisema hayo Padre Wuilliam José Vázquez Toro, wa Seminari ya Mtakatifu Petro mtume huko La Guaira, nchini Venezuela,akizungumza na Vatican News baada ya Tetemeko la ardhi lililosababisha vifo vingi katika nchi hiyo mnamo tarehe 24 Juni 2026, na kuendelea na pia kuharibu vibaya vifaa vya seminari hiyo. Huko La Guaira, shughuli za uokoaji zinaendelea bila kusita, juma moja baada ya tetemeko la ardhi, katika juhudi za kupata manusura wengi iwezekanavyo.
Idadi ya vifo vya kusikitisha imezidi watu 1,900, huku zaidi ya 10,000 wakijeruhiwa. Takriban watu 50,000 bado hawajulikani walipo na wanahofiwa kufariki. Takwimu rasmi pia zinaripoti karibu watu 16,000 waliohama makazi yao au walioathiriwa na janga hilo, huku majengo 855 yakiharibiwa. "Kuna maeneo ambayo yatalazimika kuangaliwa upya katika siku zijazo, hasa kuhusu kuhamishwa kwa wakazi wote na manusura kwenda maeneo mengine," Padre Vázquez alizungumza na Vatican News. "Kulikuwa na mazungumzo kuhusu idadi kubwa sana ya majengo ambayo yameanguka, na matetemeko ya ardhi yanaendelea. Kwa sababu ya matetemeko haya ya ardhi, watu wamehimizwa kuwa watulivu lakini pia kuwa waangalifu sana, kwani kuna maeneo ambayo yanaweza kuangukia. Sasa kazi kubwa zaidi inaanza: kuwasaidia watu kupitia hali hii," alisema.
Tumaini katika juhudi za uokoaji
Padre Vázquez akizungumza na Vatican News alielezea kwamba "watu bado wanaokolewa. Kwa mfano, jana usiku, karibu na seminari yetu, mvulana wa miaka 12 alitolewa akiwa hai kutoka kwenye kifusi, ingawa tetemeko la ardhi lilitokea Jumatano iliyopita usiku." "Tuko hapa kusaidia na kuandamana na watu. Kumekuwa na ushirikiano mkubwa. Tumeuona katika timu za uokoaji ambazo zimefika kutoka sehemu zingine na katika nguvu na ustahimilivu wa watu wa Venezuela," Padre Vázquez alisema. Pia alilalamika kwamba wanachama wengi wa mashirika ya Caritas ya parokia ya Kanisa la eneo hilo wamekufa au bado hawajulikani waliko. Hata hivyo, "Kanisa kwa sasa lina vituo vya ukusanyaji na usambazaji wa misaada huko La Guaira na katika maeneo mengine kadhaa. Vifaa vinasambazwa katika maeneo yaliyoathiriwa, hasa kufikia jamii ambazo zimeathiriwa na uharibifu mkubwa na wale walio na uhitaji mkubwa."
Jimbo la La Guaira limeachwa bila seminari
Mkuu wa Seminari ya Mtakatifu Petro Mtume pia aliripoti kwamba jengo lenyewe lilipata uharibifu mkubwa. "Karibu tumeachwa bila seminari kwa sababu, baada ya tathmini ya jengo hilo, kuna uwezekano mkubwa kwamba hatutaweza kurudi huko. Liko katika hali mbaya sana. Hata hivyo, seminari ni sisi," alisema. Pia alisifu ujasiri wa waseminari, ambao walishiriki haraka katika juhudi za kutoa misaada kwa wale walioathiriwa na janga hilo. "Niliwaambia kwamba hii inaonyesha kwamba, Mungu akipenda, watakuwa mapadre wazuri. Niliwakumbusha kwamba seminari ni kila mmoja wao, na kwamba huu ndio wakati wa kuthibitisha tena wito wa Mungu wa kumtumikia Kristo na kutumikia Kanisa." Bila vifaa vya malezi yao huko La Guaira, waseminari hao wamekaribishwa na Seminari ya huko Mtakatifu Rosa wa Lima katika mji mkuu wa Venezuela, ishara ambayo Padre Vázquez aliielezea kama "tendo kubwa la mshikamano na jimbo la kikanisa la Caracas."
Hali ya kibinadamu inazidi kuwa mbaya
Kamishna Mkuu wa Wakimbizi wa Umoja wa Mataifa (UNHCR), shirika ambalo linaratibu juhudi za ulinzi na makazi kwa wale waliohamishwa kutokana na tetemeko la ardhi nchini Venezuela, alisema tarehe 2 Julai 2026 kwamba hali ya kibinadamu katika maeneo yaliyoathiriwa "imezorota kwa kasi. Kulingana na shirika hilo, kuna "uhaba mkubwa wa chakula, kuporomoka kwa huduma za msingi, na hatari zinazoongezeka za ulinzi kwa idadi ya watu waliohamishwa."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.