Papa Leo na chama cha Mons.Courtney:Dumisheni matumaini ya Ulimwengu bora
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Papa Leo alikutana na wanachama wa Udugu wa Askofu Mkuu Courtney tarehe 22 Oktoba 2025, wakitoka Nchini Burundi. Hawa ni wanachama walianzishwa kukumbuka Askofu Mkuu Michael Aidan Courtney ambaye kunako tarehe 29 Desemba 2003 akiwa na umri wa miaka 58 alipigwa risasi kadhaa wakati akisafiri katika gari katika mji mkuu wa Nchi. Kwa njia hiyo Papa alianza na salamu kwa Askofu Mkuu Dieudonné Datonou, Balozi wa Vatican nchini Burundi, na kuwakaribisha wote wakiwa katika fursa ya hija ya jijini Roma. Kwa kumbukumbuka maneno ya kilatini ya “Spes non confundit – kwa yaani Matumaini hayakatishi tamaa (Rm 5,5), iliyochaguliwa kuongoza mwaka Mtakatifu 2025, Papa Leo XIV alieleza kwamba: “Hivi ndivyo Papa Francisko alivyotuletea Jubilei hiyo.
Tumaini letu ni Yesu Kristo! Yeye, na Yeye pekee, ndiye Tumaini la Kanisa na la ulimwengu mzima! Sote tunafahamu kwamba ulimwengu wa leo unahitaji tumaini hili; ndio maana tunasafiri kama mahujaji kukutana naye na kumweka katikati ya maisha yetu na maisha ya dunia. Kwa hiyo Papa alionesha kuwa furaha kuwakaribisha katika hija yao ya imani yao kwamba: “mtarudi kwenye ahadi zenu za kila siku mkiwa mmeimarishwa kwa matumaini, mkiwa tayari kufanya kazi kwa ajili ya maendeleo kamili ya kila mtu katika mwanga wa Injili.
Baba Mtakatifu alipenda kuwashukuru kila mmoja wao kwa nia na kujitolea kwao kwa walio hatarini. Kwa njia hiyo wanaheshimu kumbukumbu ya Askofu Courtney, ambaye alijitolea kwao na kutoa maisha yake kwa amani katika taifa lao pendwa. Katika kumbukumbu yake, wao ni familia iliyo karibu na Papa nchini Burundi, inayotamani kuwa na utume pamoja na maskini na wadogo, katika jina la Kristo. Mchango wao katika ujenzi wa mnara huko Minago—mahali alipouawa—pamoja na kuhusika kwao katika mpango wa kujenga kituo cha afya, kazi zao za kila siku za upendo kwa wale wanaohitaji sana, na mipango mingine mingi, ni ujumbe wenye nguvu kwa Kanisa katika nchi yao.
Papa aliwageukia wanachama hao wa Udugu wa Askofu Mkuu Courtney akiwashukuru kwa ziara yao na kuwahakikishia kuwatia moyo kwa dhati kwa kuendelea na shughuli zao. Aliwambia kwamba wadumishe tumaini la ulimwengu bora; “kwa kudumisha uhakika kwamba, kwa kuunganishwa na Kristo, juhudi zao zitazaa matunda na kupata thawabu. Papa Leo aliwakabidhi wao na Nchi yao Pendwa ya Burundi, kwa ulinzi wa Mama Yetu wa Rozari, na kwa moyo mkunjufu alitoa Baraka yake ya Kitume, na ambayo ametoa kwa familia zao, wafadhili wanaofanya kazi kwa ajili ya maendeleo fungamani ya watu wa Burundi.
Asante kwa kusoma makala hii. Kama unataka kubaki na sasisho, basi bonyeza hapa: Just click here
