Papa,Vyombo vya habari:Mnasaidia Papa na Vatican kuwasilisha Habari Njema Ulimwenguni!
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Jumamosi alasiri tarehe 11 Oktoba 2025 kwa Jumuiya ya wafanyakazi wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano, ilikuwa ni wakati muhimu wa mtindo wa kifamilia kuwa pamoja katika eneo ambalo Radio Vatican ilianzishwa kunako mwaka 1931. Ni katika fursa hiyo, ambapo Papa Leo XIV aliweza kufika kukutana na kusalimiana na Wafanyakazi wa vyombo vya habari vya Vatican wakiwa na familia zao, mbele ya Jumba dogo la Leo XIII katika bustani za Vatican. Baada ya kufika na kukaribishwa na Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano, Dk. Paolo Ruffini, Baba Mtakatifu alianza hotuba yake huku akishukuru na kusalimia. Baadaye Papa alisema : Nimefurahi kuwa nanyi kidogo, ninyi ambao mnaunda Jumuiya kubwa ya kazi ya Baraza la Kipapa la mawasiliano.”
Baba Mtakatifu aliendelea: “Leo ninawaona nyinyi, kwa njia ya kusema, katika “muundo wa familia,” na ninafurahi pamoja nanyi kwa sababu Kanisa ni familia, familia ya kifamilia. Ninafurahi pia kukutana nanyi mahali hapa, ambapo panatukumbusha kumbukumbu ya Papa Leo XIII, hasa umakini wake kwa njia za mawasiliano ya kijamii.” Papa aliongeza kusema: “Mnatoka nchi nyingi. Lugha mlizojifunza mkiwa watoto ni tofauti, na pia mnafanya shughuli tofauti. Lakini aina hizi zote zimewekwa kwenye huduma ya lengo moja la: kusaidia Papa na Kiti kitakatifu kuwasilisha Habari Njema Ulimwenguni kote.”
Kama Mtakatifu Paulo anavyoandika katika Waraka wa Kwanza kwa Wakorintho, Papa aliongeza, “kuna karama mbalimbali, lakini Roho ni yule yule; pana tofauti za huduma, lakini Bwana ni yeye yule; kuna shughuli mbalimbali, lakini Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika kila mtu (taz.12:4-6).” Kwa njia hiyo Baba Mtakatifu alitoa sifa kwa wafanyakazi kwamba , “Nawapongeza kwa mtandao ambao mmekuwa mkiujenga ndani ya Baraza la Kipapa kwa miaka mingi; na pia kwa sababu mnafanya hivyo, kama Papa Francisko ambavyo angesema: "kutoka nje” yaani, kutupa wavu huu kati ya Vatican na Ulimwengu, "kutweka hadi kilindini, hadi mwisho wa dunia.”
Papa Leo alisisitiza kuwa “Kwanza kabisa ni mtandao wa watu, kila mmoja akiwa na ujuzi wake, unaotolewa kwa Kanisa. Ni mtandao unaotolewa kwa ulimwengu kushirikisha ukweli, kusaidia watu kuona na kuelewa, na daima kwa upendo. Ni mtandao ambapo majukumu ni tofauti, lakini ambao hakuna umuhimu zaidi kuliko mwingine.”
Papa kwa kukazia zaidi alibanisha kwamba “ Ninaanza kuwafahamu taratibu. Ninajua mnafanya kazi kwa bidii kueneza maneno na ishara za Papa kila mahali. Mnafanya kila siku, kwa busara na kujificha.” Papa wa Roma alisisitiza tena kwamba: “Lakini leo hii nina furaha kwa sababu nimepata fursa ya kuwaona, kukutana nanyi, hasa katika mazingira haya ya familia, sote kwa pamoja.”
“Nimeambiwa kwamba mnakutana kila mwaka kwa njia rahisi kwa picnic. Hii ni nzuri sana: kwani pamoja na kazi, mnaweza kushiriki wakati wa kupumzika na sala. Na wakati huu mlitaka kufanya hivyo leo hii, ili baadaye muweze kufika kwenye Uwanja wa Mtakatifu Petro kusali pamoja kwa ajili ya amani.” Papa aliongeza tena “Ndiyo, jinsi gani ilivyo muhimu kwamba mawasiliano yetu yaambatanishwe na sala! Ningesema hii inaleta tofauti zote. Ulimwengu unaweza usiujue, hauwezi kuuelewa, lakini sisi tunaelewa, na lazima tujitahidi kufanya hivyo kila wakati: kusindikizana kwa sala katika kazi yetu ya kila siku ya mawasiliano.”
Papa kwa kuhitimisha alitoa shukrani tena akisema: “Wapendwa, asante kwa wakati huu mzuri! Ninawabariki ninyi nyote kwa upendo, hasa watoto na wapendwa wenu ambao ni wagonjwa. Mama Yetu awasaidie na kulinda familia zenu. Asanteni nyote! Kwa hiyo, pamoja na wadogo zaidi, pamoja na wakubwa zaidi, sote tunajua kwamba Mungu ni Baba, na hivyo na tusali pamoja kama Yesu alivyotufundisha.” Baba Yetu Uliye Mbinguni…
Papa aliongoza sala ya Baba Yetu na baraka.”
