Papa Leo XIV kwa wanahija kutoka Kroatia:Imani hukua na kuongezeka ikishirikishwa
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV aliwakaribisha Wakroatia 10,000 waliokusanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Petro Jioni tarehe 7 Oktoba 2025 Mama Kanisa akiwa anaadhimisha Siku Kuu ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu, ambao, wakiwa wamefika Roma hivi karibuni kwa ajili ya hija ya kitaifa kwa Mwaka Mtakatifu 2025. Papa, baada ya kurejea kutoka Castel Gandolfo, mara moja alitoa hotuba fupi kwa waamini, ambao Askofu Mkuu Dražen Kutleša wa Zagreb aliadhimisha Misa, kwa kushirikisha maaskofu na mapadre kadhaa. Kabla ya kufika uwanjani mbele ya Basilika ya Vatican, Papa Leo alipanda gari la kipapa, na kuwazungukia wanahija hao huku akitoa salamu na tabasamu, akisimama mara kwa mara ili kuwabariki watoto na kunyakua mitandio, bendera, na zilizorushwa kwa heshima yake.
Papa Leo XIV alianza na salamu “ Tumsifu Yesu Kristo na Maria, hata kutamka lugha yao “Hvaljen Isus i Marija! Wapendwa mahujaji wa Kroatia, ninawakaribisha kwa furaha kuu katika Uwanja wa Mtakatifu Petro, ambapo mmekusanyika kwa ajili ya hija yenu ya kitaifa katika Mwaka wa Jubilei. Uwepo wenu kwa wingi na wa maombi ni ishara fasaha ya uchangamfu wa imani ya watu wenu, ambao kwa karne nyingi wamebaki thabiti katika ushirika na Kanisa na waaminifu kwa Mrithi wa Mtume Petro. Ni jambo la kutia moyo sana kuona kwamba mizizi ya imani yenu haijabaki palepale hapo awali, bali inaendelea kuzaa matunda hata leo hii, shukrani kwa ushuhuda wa familia zenu, jumuiya za parokia zenu na mashirika yenu.” Baba Mtakatifu Leo XIV aliendelea kusema kuwa “Mapokeo yaliyorithiwa kutoka kwa mababu zenu ni hazina ya thamani, ambayo mnailinda kwa uangalifu na ambayo mmeitwa kuzidisha upya, daima mkiwa wazi kwa kutambua uvuvio wa Roho Mtakatifu.Ninawashukuru kwa moyo wangu kwa uaminifu huu mnaoishi kwa uthabiti wa maisha ya kila siku.”
Papa alielezea anavyojua kwamba wengi wao wanajikuta katika sehemu mbali mbali za dunia, kwa kufukuzwa mbali na nchi yao, kutoka kazini, kusoma, au kutokana na mahitaji mengine; lakini popote pale walipo, waendelee kushikamana na mizizi yao ya Kikristo na kutoa ushuhuda wa watu wanaompenda Kristo na Kanisa lake. Mshikamano huu wa maisha ni neno la Injili lenye ufasaha zaidi kuliko hotuba nyingi. Papa amewatia moyo daima wakaze macho yao kwa Yesu, Mchungaji Mwema, anayewaongoza na kuwasindikiza, na kujiruhusu kuongozwa naye kwa uaminifu na unyenyekevu. Wasisahau kwamba imani hukua na kuimarika inaposhirikiswa: kwa hiyo, Papa ametoa mwaliko kuwa “Ninawaalika kuwarithisha watoto wenu na vizazi vipya maadili ya Kikristo ambayo yameunda historia yenu ndefu na utamaduni wenu.”
Kwa njia hii, Papa alisisitiza kwamba wataendelea kuwa chachu ya amani, wema, na matumaini katika ulimwengu uliosambaratishwa na vurugu na vita, ambao pia wanaujua kutokana na historia yao. Bwana awabariki, na Bikira Maria wanayemwita kama Advocata fidelissima Croatiae, yaani Wakili mwaminifu wa Kroatia awalinde chini ya vazi lake na kuwasindikiza katika safari yao ya kila siku. Kwa wote waliokuwapo, kwa familia zao, kwa wapendwa wao wote, na kwa watu wote wa Kroatia, amewapa kwa moyo wote Baraka ya Kitume, ishara ya ukaribu na upendo wa Papa kwa kila mmoja wao. Baada ya Salamu Hizo Papa alitanguliza sala ya baba Yetu kwa lugha ya Kilatini:
“Oremus,”…Tuombe: ….Pater Noster
Baraka...
Asante sana kusoma makala hii. Kama unataka kusasishwa zaidi, jiandikishe katika makala za kila siku kwa kubonyeza hapa: Just click here
