Papa Leo XIV:Maria kwa tumaini,Mungu anatimiza ahadi zake
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV jioni, Jumatatu tarehe 6 Oktoba 2025 aliongoza Masifu ya kwanza ya jioni katika Kanisa la Mama Yetu wa Rozari wa Pompei na Mtakatifu Petro Chanal wa Nyumba (Domus)ya Australia iliyoko Roma, katika fursa ya Siku Kuu ya Mama Yetu wa Rozari wa Pompei. Kabla ya kuondoka alibariki picha ambayo ilichorwa miaka ya 1800 na Mtakatifu wa baadaye Bartolo Longo. Hiyo ni nyumba ambayo Mama Maria wa Rozari ni Msimamizi wake wa watawa kwa ajili ya mapumziko, hatua chache kutoka kituo kikuu cha Treni kiitwacho Termini, ambapo Papa alifika miada ya saa 11.45 njioni na kupokelewa na shangwe na umati iliokuwa njia ya Cernaia. Baba Mtakatifu aliingia ndani ya Kanisa akisindikizwa na Wimbo wa “Wewe ni Petro”(Tu es Petrus,)ulioimbwa na Kwaya “The Gradualia Consort.”
Katika mahubiri ya masifu hayo, Papa Leo alianza kusema kuwa: “Nimefurahi kuwa nanyi kwa ajili ya kusherehekea Masifu ya Kwanza mnapoadhimisha Sikukuu yenu ya Mlinzi Mama Yetu wa Rozari wa Pompei. Kwa hakika, ibada hii kwa Mama Yetu Mbarikiwa ina nafasi ya pekee moyoni mwangu, kwa hiyo nina furaha pia kushiriki tukio hili na jumuiya ya Australia iliyopo kwa ajili ya baraka hii ya dhati ya Picha iliyokarabatiwa ya Mama Yetu wa Pompei.” Papa akiendelea alisema kuwa “Ni matumaini yangu kwamba picha hii, ambayo ilitolewa kwa ajili ya kanisa hili miongo mingi iliyopita na Mtakatifu Bartolo Longo ambaye hivi karibuni atatatangazwa rasimi kuwa Makatifu, itatia moyo wa kujitolea zaidi kwake miongoni mwa wakazi wa Nyumba hii (Domus) na wale wanaotembelea kama mahujaji, pamoja na wanajumuiya wa mahali hapo.”
Kimaandalizi, Papa alisema “tumekusanyika pamoja katika Mwaka huu wa Jubilei, ambao unazingatia fadhila ya kitaalimungu ya Matumaini. Kwa namna fulani, Maria alitia ndani wema huo kupitia tumaini lake kwamba Mungu angetimiza ahadi zake.” Tumaini hili, kwa upande wake, lilimpatia nguvu na ujasiri wa kutumia maisha yake kwa hiari kwa ajili ya Injili na kujiachia kabisa kwa mapenzi ya Mungu. Imesemwa mara nyingi kwamba Umwilisho ulifanyika kwanza katika moyo wa Maria, kabla haujatukia katika tumbo lake la uzazi. Hii inasisitiza uaminifu wake wa kila siku kwa Mungu. Bila shaka, Maria hakujua hususani jinsi au lini Mungu angewaokoa watu wake, lakini aliishi kwa kufanya mapenzi ya Mungu, akitumaini kwamba angewaokoa watu wake kulingana na mpango wake. Mungu hachelewi, sisi ndio tunapaswa kujifunza kuamini, hata ikihitaji uvumilivu na ustahimilivu.
Papa Leo alibainisha kwamba wakati wa Mungu daima ni mkamilifu. Kwa hivyo, "tulisikia katika kifungu cha Maandiko kutoka Mtakatifu Paulo, "wakati uliowekwa ulipofika, Mungu alimtuma Mwanawe ili kuwakomboa walio chini ya sheria." Kwa njia hiyo Papa aliongeza: "Mungu daima huja kutuokoa na kutukomboa. Waisraeli walizaliwa chini ya sheria lakini pia na udhaifu, na tamaa ya hali yetu ya kuanguka ya kibinadamu." Mpango wa Mungu kwa hiyo - sasa umetimizwa katika utume wa Bwana Yesu. Zaidi ya hayo, hakuja ili tu kutukomboa kutoka katika utumwa wa dhambi, bali kuikomboa mioyo yetu ili iseme ‘ndiyo’ kwake, kama vile Mama Yetu Maria alivyofanya."
Sasa kupitia zawadi ya ubatizo, tunazaliwa chini ya sheria ya neema kama watoto wa Mungu. Katika maneno ya Wimbo wa Sifa, Mungu Baba yetu “alituchagua katika Kristo kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu … alituchagua katika upendo tuwe wana na binti zake katika Yesu Kristo, sawasawa na kusudi la mapenzi yake.” Kusudi la mapenzi yake ni kutupeleka pamoja kwenye uzima wa milele. Kuhusiana na hili, Mtakatifu Agostino aliandika kwamba, "Mungu alituumba bila sisi, lakini hatatuokoa bila sisi." Hivyo, tunaitwa kushirikiana naye kwa kuishi maisha ya neema kama wana na binti zake, tukitoa mchango wetu wenyewe kwa mpango wa wokovu. Hii ni kweli ingawa hatujui wakati ujao una nini. Hata hivyo, kama Maria, tunaweza daima kuwa wenye kutumainika na wenye shukrani kwa ajili ya kazi yake ya wokovu.
Papa Leo XIV aliwakumbusha jinsi ambavyo muda mfupi wangeimba Wimbo wa Sifa wa Maria yaani wa "Magnificat.” Kwa kufanya hivyo, “ni kutafakari jinsi Maria, Binti Sayuni wa kweli, alivyomfurahia Mungu, Mwokozi wake, kwa sababu aliona neema alizopewa na jinsi Mungu amekuwa mwaminifu kwa Ibrahimu na kizazi chake.” Na kwa njia hiyo aliwaeleza kwamba wanapommheshimu Mama Yetu wa Pompei katika Nyumba hiyo ya Australia, ni maombi yake kwamba wao pia wataimarishwa na Roho Mtakatifu katika huduma yao kwa Bwana na Kanisa lake, na kwamba wapate kuzaa matunda mengi, matunda yatakayodumu, alihitimisha.
