Papa Leo XIV:Utambulisho wa Kikristo ni dira ya elimu
Vatican News
Katika ujumbe kwa njia ya video kwa mkutano wa "Sin identidad no hay educación" yaani "Bila utambulisho hakuna elimu" katika Chuo cha Mama Yetu wa Shauri Jema, huko Madrid Jumamosi tarehe 22 Novemba 2025, Papa Leo XIV aliwasifu waelimishaji kwa kujitolea kwao katikati ya changamoto za elimu ya kisasa. "Dhamira yenu katika huduma ya Kanisa ni chachu hai kwa vizazi vipya na jamii zinazopata ndani yake sehemu muhimu ya marejeleo," Papa alisema. Akisisitiza mada ya mkutano huo, Papa alibainisha kuwa "bila utambulisho, hakuna elimu." Alielezea kwamba utambulisho wa Kikristo si nembo ya mapambo, bali "kiini hasa kinachotoa maana, mbinu, na kusudi kwa mchakato wa elimu."
Dira ni Kristo
Papa aliendelea kueleza kuwa, “Kama vile mabaharia wanavyotegemea Nyota ya Kaskazini, katika elimu ya Kikristo dira ni Kristo. Bila mwongozo huu, elimu ina hatari ya kuwa ya kawaida na kupoteza nguvu zake za mabadiliko.” Pia alisisitiza ujumuishaji wa imani na mantiki katika elimu. "Sio nguzo zinazopingana bali ni njia zinazosaidiana kuelewa uhalisia, kuunda tabia, na kukuza akili. Uzoefu wa kielimu lazima uhusishe sayansi na historia, maadili na kiroho, yote ndani ya jamii ambayo ni kama nyumba. Ushirikiano wa kweli kati ya familia, parokia, shule, na hali halisi za ndani huambatana na kila mwanafunzi kwa njia halisi katika safari yao ya imani na kujifunza," alisema.
Jukumu la Mama la Kanisa katika elimu
Alikumbusha zaidi jukumu la mama Kanisa katika elimu, kama ilivyoelezwa na Mtaguso wa Pili wa Vatican. "Kanisa ni mama anayezalisha waamini, mwenzi wa Kristo. Linalinda uwezo wa kuongoza na kufundisha, uliokabidhiwa kwake na Mwanzilishi wake mtakatifu zaidi: kuzaa watoto, kuwaelimisha, na kuwaendeleza, kuongoza kwa maongozi ya mama maisha ya watu binafsi na watu."
Gravissimum educationis
Hatimaye, akiashiria kumbukumbu ya miaka 60 ya tamko la Mtaguso wa II wa Vatican la Gravissimum educationis, uliojikita kuhusu Elimu ya Kikristo na ambao ulihamasisha mafunzo na malezi ya kibindamu kwa misingi ya wema wake na binadamu wote. Kwa hiyo Papa Leo XIV aliwahimiza waelimishaji kuona kazi yao kama sehemu ya dhamira muhimu ya Kanisa. "Elimu si huduma ya kijamii tu, bali ni usemi wa utambulisho na wito wa Kanisa," alisema.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here
