Papa Leo XIV:Ekaristi ni Mkate wa safari,unaotuongoza kuelekea nchi ya mbinguni
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV aliwasalimia na kuwakaribisha waamini na mahujaji kutoka ulimwengini kote, waliokusanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumatano tarehe 24 Juni 2026 siku ambayo, Mama Kanisa anaadhimisha sherehe za Mtakatifu Yohane Mbatizaji. Katika kuanza aliwaeleza kuendelea na Katekesi kuhusu Hati za Mtaguso wa II wa Vatican kwa namna ya pekee juu ya Katiba ya Sacrosanctum Concilium (SC) kuhusu Liturujia. Papa Leo XIV alisema kuwa “Mtakatifu Augustino anapotaka kuwaelezea fumbo la Mwili wa Kristo waliokuwa wamebatizwa karibuni, alianza na kifungu kutoka kwa Mtakatifu Paulo ambacho tumesikia: "Ninyi ni mwili wa Kristo na kila mmoja kwa sehemu yake, viungo." (1Kor 12,27). Na aliongeza: "Ni siri yako unayopokea. Kwa kile ulicho, unaitikia: Amina, na jibu lako ni kama sahihi yako. Unaambiwa: 'Mwili wa Kristo,' na unaitikia: 'Amina.' Kwa hivyo, iweni viungo vya mwili wa Kristo, ili amina yenu iwe kweli. […] Kuwa kile mnachokiona, na kupokea kile mlicho" (Mahubiri 272: PL 38, 1247).
Kuburudhiwa mezani na Mwili wa Bwana
Mara tu baada ya kukumbuka Karamu ya Mwisho ya Yesu, Katiba ya Liturujia inazungumzia Ekaristi kwa misemo hii ya Augustino. Kwa Wakristo, kushiriki katika meza ya Bwana kunamaanisha "kuumbwa kwa Neno la Mungu, kuburudishwa mezani na Mwili wa Bwana, tukimshukuru Mungu" (tazama SC, 48). Ni kwa kumpokea katika Neno Lake na katika Ekaristi ndipo tunakuwa kile tunachopokea. Tunakuwa Mwili ambao Kichwa chake ni Kristo aliyefufuka, ameketi mkono wa kuume wa Baba (taz. Kol 1:18), ambaye anatuandalia mahali mbinguni (taz. Yoh 14:3): Ekaristi kwa hivyo ni sakramenti ya Ufalme ujao.
Mkate wa safari unaotuongoza nchi ya mbinguni
"Ni Mkate wa safari, unaotuongoza kuelekea nchi ya mbinguni, hadi siku iliyobarikiwa ambapo "Mungu atakuwa yote katika wote" (1 Kor 15:28). Kusanyiko la kiliturujia hutoa Sadaka "sio tu kupitia mikono ya Padre , bali pia katika muungano naye" (SC, 48). Kwa mtazamo huu, Ekaristi ni aina ya sadaka ya kiroho ya Wakristo (taz. Ebr 13:16; Rum 12:1), kama njia ya kuungana na Mungu na wao kwa wao. Kwa kushiriki katika hilo, wanajifunza "kujitoa wenyewe na siku baada ya siku, kulishwa, kupitia Kristo, katika umoja na Mungu na wao kwa wao," kwa hivyo, kwa kutuingiza katika Kristo, Ekaristi inatufundisha kuiga mtindo wa maisha wa Bwana Yesu mwenyewe, unaoonyeshwa na zawadi ya bure ya nafsi. Papa aliendelea kuwa, kwa njia hiyo “zawadi hii inaturuhusu kuingia katika nguvu ya umoja, ambayo hutoa dawa yenye nguvu ya migawanyiko inayoharibu ulimwengu wetu, jamii zetu, familia zetu, na mioyo yetu (tazama SC, 47). Papa alibainisha kwamba “, tunaposhiriki katika misa , tunaalikwa kusikiliza Neno la Mungu na kulishwa mezani pa Bwana, ambapo anajitoa kwa Baba.
Sehemu mbili za Misa:Liturujia ya Neno na Liturujia ya Ekaristi
Papa alisisitiza kwamba "Sehemu hizi mbili za Misa, Liturujia ya Neno na Liturujia ya Ekaristi, "zimeunganishwa kwa karibu sana kiasi kwamba zinaunda tendo moja la ibada" (SC, 56). Kuhusu Neno, ni lazima ikumbukwe kwamba si suala la kupata maarifa ya kiakili ya Maandiko Matakatifu tu, bali ni la kupokea Neno "lililo hai na linalofanya kazi" (Ebr 4:12), linaloelekezwa na Mungu kwa kila mmoja wetu, Neno linalolisha na kulisha, pamoja na Mkate wa Ekaristi, na kutuongoza kutoka kwenye uharibifu wa dhambi hadi kwenye maisha mapya katika Kristo. "Ekaristi inatufungulia uelewa wa Maandiko Matakatifu, kama vile Maandiko Matakatifu yanavyoangazia na kuelezea Fumbo la Ekaristi"(Benedikto XVI, Wosia wa Kitume wa Baada ya Sinodi Verbum Domini, 55).
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ulitoa wito wa kufunguliwa kwa hazina za Biblia kwa ukarimu zaidi, ili meza ya Neno la Mungu itolewe kwa waamini kwa wingi zaidi (taz. SC, 51). Mageuzi ya kiliturujia yalitafsiri ombi hili kuwa hazina ambayo ni Kitabu cha Masomo, kitabu kinachokusanya masomo yote ya Biblia kwa ajili ya sherehe za kiliturujia. Upana huu wa masomo ulichukuliwa kutoka chanzo safi kabisa cha Mapokeo hai, ambayo huchanganya uaminifu kwa mapokeo na uwazi kwa mchakato halali (taz. SC, 23).
Mto wa Mapokeo unaotiririka hadi kwetu
Mwanzo wa Sura ya II ya Katiba kuhusu Liturujia imeunganishwa na marejeo ya mto mkubwa wa Mapokeo, unaotiririka kutoka kwa Mababa wa Kanisa hadi kwetu: "Katika Karamu ya Mwisho, usiku aliosalitiwa, Mwokozi wetu alianzisha sadaka ya Ekaristi ya mwili na damu yake, ili kuendeleza sadaka ya msalaba katika karne zote hadi atakaporudi, na hivyo kumkabidhi bibi harusi wake mpendwa. Papa Leo XIV alisisitiza kwamba Kanisa, ukumbusho wa kifo chake na ufufuo: sakramenti ya upendo, ishara ya umoja, kifungo cha upendo, karamu ya pasaka, ambapo Kristo analiwa, roho imejaa neema, nasi tunapewa ahadi ya utukufu ujao" (SC, 47). Kwa kuhitimisha Papa aliwaomba kuwa “ kaka na dada wapendwa, hebu tujitoe kwa imani kutoka kwenye chanzo hiki cha uzima wa kimungu na tujiachie tubadilishwe na fumbo tunalosherehekea.”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here.
