Papa Leo XIV:Kuishi kunamaanisha kujifunza kuishi kwa amani na wengine!
Na Angella Rwezaula - Vatican.
Kwa wanariadha kutoka ulimwenguni watakaoshiriki Toleo la 62 la Kombe la Kuogelea la "Sette Colli" mjini Roma katika siku zijazo, Baba Mtakatifu Leo XIV alibainisha kuwa hii ni "ishara ya matumaini, ishara ya ulimwengu tunaoutaka." Papa alikutana nao pamoja na viongozi wa Shirikisho la Kuogelea la Italia Alhamisi asubuhi tarehe 26 Juni 2026 katika Ukumbi wa Clementine mjini Vatican, wakati wa Mashindano ya Kimataifa ya Kuogelea, yatakayofanyika kuanzia tarehe 25 - 28 Juni 2026 katika Ukumbi wa Foro Italico.
Mchezo unachangia ukuaji wa kiroho
Papa Leo XIV alisema kwamba "Nyinyi nyote, kiukweli, kutoka nchi tofauti, mmekusanyika hapa, mkiongozwa na shauku ile ile na maadili yaleyale, zaidi ya tofauti yoyote ya lugha, utaifa, au utamaduni. Ukweli huu, wa kawaida wa matukio ya michezo ya kimataifa, unatoa ishara ya matumaini, ishara ya ulimwengu tunaoutaka; unachangia makutano ya amani kati ya watu na udugu."
Papa Leo XIV alisema, "wakati mazoezi yanafanywa vizuri," huendeleza ukuaji wa "viungo mbalimbali vya mtu," ikithamini "kujitolea, mshikamano, na uaminifu." Zaidi ya hayo, si dawa ya mwili na roho tu, bali pia fursa ya ukuaji wa kiroho. Kwa njia hiyo kuogelea, hasa, kwa kuogelea majini, kwa mfano hukumbusha kipengele cha msingi cha ubinadamu.
Kueneza maadili ya michezo
Papa Leo XIV alisisitiza kwamba "Kuishi kunamaanisha kujifunza kuishi kwa amani na wengine na mazingira yanayotuzunguka. Kwetu sisi Wakristo, maji ni ishara ya Ubatizo na maisha mapya katika Kristo." Kadhalika Papa aliwahimiza wanariadha kuendelea "kufanya mazoezi na kueneza" maadili ya michezo, hata zaidi ya taaluma zao: "Umri wa michezo ya ushindani hupita, lakini maadili hayo hubaki!" Hatimaye, aliwakabidhi wote kwa maombezi ya Mtakatifu Pier Giorgio Frassati, "mwanariadha kijana aliyependa kupanda milima sana."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here.
