Papa Leo XIV: Kutabarukiwa Kwa Kanisa Kuu la Bikira Maria Mkuu, Jimbo kuu la Roma
Na Padre Richard A. Mjigwa C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV wakati wa Katekesi yake Kuhusu Waraka wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican: “Sacrosanctum concilium” yaani “Juu ya Liturujia” amechambua kuhusu: “Sala ya Kanisa Katika Liturujia” na kuwakumbusha waamini kwamba, Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 5 Agosti, anaadhimisha Kumbukizi ya Kutabarukiwa kwa Kanisa la Bikira Maria Mkuu lililoko Jimbo kuu la Roma. Baba Mtakatifu Leo XIV anawaalika waamini kumwomba Bikira Maria awasaidie kuwa waaminifu katika maisha ya sala kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mwenyezi Mungu. Hili ni Kanisa lililojengwa kwa heshima ya Mama wa Mungu mara baada ya Mtaguso wa Efeso, uliofanyika kunako mwaka 431, hapo Kanisa likamtangaza Bikira Maria kuwa ni "Theotokos" yaani Mama wa Mungu. Kanisa hili ni chimbuko la utajiri na amana ya Fumbo la Umwilisho, Neno wa Mungu alipofanyika mwili na kukaa kati ya waja wake. Kanisa hili pia linatunza masalia ya Sanamu ya Bikira Maria Afya ya Warumi “Salus Populi Romani”, faraja ya wale wote wanaomkimbilia Bikira Maria kwa imani na matumaini katika shida na mahangaiko yao ya ndani! Huu ni mwaliko wa kumtafakari Bikira Maria, Afya ya Warumi! Kanisa hili ni ushuhuda wa utenzi wa Bikira Maria, “Magnificat” aliposema “Kwa maana, tazama, tokea sasa vizazi vyote wataniita mbarikiwa kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea makuu na jina lake ni takatifu.” Lk. 1:47. Ujumbe huu wa Bikira Maria umepokelewa na waamini wa vizazi vingi, wanaofika kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mkuu, ili kuadhimisha Sakramenti mbalimbali za Kanisa. Kanisa hili limekuwa ni Madhabahu ya kwanza yaliyojengwa kwa heshima ya Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa kwa nchi za Magharibi. Madhabahu haya ni mahali ambapo waamini wanapata fursa ya kusikiliza Neno la Mungu, Kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa na kujipatia neema ya toba na wongofu wa ndani, tayari kuandika upya historia ya maisha yao. Kwa wale waliopondeka na kuvunjika moyo, wanaweza kupata faraja kutoka kwa Bikira Maria, Afya ya Warumi.
Tukio hili limeadhimishwa kwa sala ya siku tatu mfululizo, “Triduo” na kuhitimishwa kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Kardinali Rolandas Makrickas, Mhudumu mkuu wa Kanisa la Bikira Maria mkuu, Jimbo kuu la Roma. Katika mahubiri yake amewaalika waamini kutafakari kwa kina Liturujia ya Neno la Mungu mintarafu Bikira Maria aliyechaguliwa kuwa ni Mama wa Mungu, Neno aliyefanyika mwili. Bikira Maria ni Hekalu hai, Sanduku la Agano Jipya na ni Nyumba ya Mungu, Tabernakulo ya kwanza ya Neno aliyefanyika mwili, mahali ambapo Mwenyezi Mungu amepachagua ili pawe ni makazi yake na kwamba, Utenzi wa Bikira Maria ni mshangao wa matendo makuu ya Mungu katika maisha na utume wa Bikira Maria, Mama mwenye kimya kikuu na mnyenyekevu ambaye kwa njia yake, Mwenyezi Mungu ametenda mambo makuu. Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Masifu ya Pili ya Jioni, tarehe 5 Agosti 2024 katika mahubiri yake alikazia kuhusu: Muujiza wa theluji kuanguka, wakati wa Mwezi Agosti; Picha ya Bikira Maria akiwa amembeba Mtoto Yesu; Watu wengi wanakimbilia ulinzi na tunza ya Bikira Maria katika shida na mahangaiko yao. Muujiza wa theluji kuanguka ni kielelezo kinachojikita katika mshangao, kielelezo cha neema na zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kimsingi neema huamsha mvuto na mshangao. Picha ya Bikira Maria akiwa amembeba Mtoto Yesu ni sehemu ya utambulisho wa Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu na kwamba, huu ni utimilifu wa neema. Hii picha inaonesha mambo msingi ya kiimani: Mwanamke na Mtoto wake. Maandiko Matakatifu yanasema: “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana.” Gal 4: 4-5.
Huyu ni mwanamke aliyejaa neema, aliyetungwa mimba bila ya kuwa na dhambi ya asili. Mwenyezi Mungu akamwangalia kwa jicho la upendeleo na kumteuwa kuwa ni Mama ya Mwanaye mpendwa. Bikira Maria ni mwanamke wa kwanza kubarikiwa, kielelezo cha utimilifu na ukuu wa Mungu. Ndiyo maana watu waaminifu wa Mungu wanakimbilia ulinzi na tunza ya Bikira Maria, chemchemi ya neema inayobubujika kutoka kwa Kristo Yesu kwa njia ya Roho Mtakatifu. Wakati huu waamini wamekusanyika kuomba ulinzi na tunza ya Bikira Maria kwa ajili ya mji wa Roma na Ulimwengu katika ujumla wake: wanaomba amani ya kudumu inayopata chimbuko lake kutoka katika mioyo iliyotubu na kusamehewa; amani inayobubujika kutoka katika Msalaba wa Kristo, kwa njia ya Damu yake Azizi kwa ajili ya maondoleo ya dhambi! Mtakatifu Cyril wa Alexandria, Askofu na Mwalimu wa Kanisa baada ya Maadhimisho ya Mtaguso wa Efeso alisikika akisali hivi: “Ninakusalimu Bikira Maria, Mama wa Mungu, Wewe uliyembeba Mwanga, Wewe ni safi. Ninakusalimia Bikira Maria, Mama na Mtumishi. Bikira Maria, ambaye kwa njia yake amezaliwa Mwana wa Mungu; Huyu ndiye uliyembeba mikononi mwako… Ninakusamilia amana na utajiri wa dunia; Taa isiyozimika; Kwako, amezaliwa mwanga wa Mataifa. Bikira Maria Mama wa Mungu, Utuombee!
