Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni Mwili na Roho: Mama Ya Sherehe Zote!
Padre Octavian Onesmo Hinju na Padre Kelvin Onesmo Mkama, Tanzania
Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican wanasema, Bikira Maria ni ishara ya Taifa la Mungu, kwani Mama wa Yesu, akiwa amekwisha kutukuzwa mbinguni mwili na roho, ni sura na mwanzo wa Kanisa ambalo litapata utimilifu wake katika ulimwengu ujao. Kadhalika anang’aa duniani kama alama ya hakika ya matumaini na ya faraja kwa Taifa la Mungu lilo safarini, mpaka siku ya Bwana itakapokuja. Rej. 2Pet 3:10. LG, 68. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema, Bikira Maria ambaye Kristo Yesu Mfufuka alimchukua mwili na roho hadi katika utukufu, anang’ara kama kielelezo cha matumaini kwa watoto wake wanaosafiri katika historia yote. Katika maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni mwili na roho, tarehe 15 Agosti 2026, Baba Mtakatifu Leo XIV, majira ya saa 4: 00 za Asubuhi sawa na Saa 5: 00 za Asubuhi, anaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu katika Parokia ya Kipapa ya “San Tommaso da Villanova” iliyoko kwenye Ikulu ndogo ya Castel Gandolfo na atawaongoza waamini na mahujaji kwa Sala ya Malaika wa Bwana. Sherehe ya Kupalizwa Bikira Maria Mbinguni mwili na roho inapata chimbuko lake katika Mapokeo ya Kanisa na hasa zaidi wakati wa Maadhimisho ya Mtaguso wa Efeso uliofanyika kunako mwaka 431, ulipotamka kuwa Bikira Maria ni Mama wa Mungu, “Theotokos.” Waamini wa Kanisa la Mashariki kwa miaka mingi walikuwa wanaiadhimisha Sherehe hii ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni mwili na roho kama kielelezo cha kulala usingizi wa amani “Dormitio, Kimisis” na wataalam wengine wakaongeza kusema, “Somnum Mariae.” Hii ni Sherehe inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila Mwaka ifikapo tarehe 15 Agosti. Mwili wa Bikira Maria uliokuwa umekingwa na dhambi ya asili, ukapalizwa mbinguni. Hiki ni kielelezo makini cha imani ya watu wa Mungu kama alivyokiri Mtakatifu Yohane Paulo II kunako mwaka 1997. Hii ni Mama wa Sherehe zote za Bikira Maria zinazoadhimishwa na Mama Kanisa na ni kama Pasaka ya Bikira Maria.
Kwa mwanga na nguvu tendaji ya Roho Mtakatifu, akiwa ameungana na Maaskofu wenzake, Papa Pio IX kunako tarehe 8 Desemba 1854 akatangaza rasmi kwamba, Bikira Maria kukingiwa dhambi ya asili ni sehemu ya Mafundisho tanzu ya Kanisa Katoliki. Bikira Maria tangu nukta ya kutungwa kwake mimba, kwa neema na upendeleo wa pekee kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kwa kutazamia mastahili ya Kristo Yesu, Mwokozi wa wanadamu wote, alikingiwa na kila doa la dhambi ya asili. Baba Mtakatifu Benedikto XVI anatukumbusha kwamba, maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni yanakwenda sanjari na Fumbo la Pasaka, yaani: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo Yesu kutoka kwa wafu. Bikira Maria, Mama wa Mungu kwa upendeleo na neema ya Mungu akabahatika kuwa ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili na hivyo kushirikishwa kwa namna ya pekee kabisa, katika Fumbo la Pasaka na utukufu wa Kristo Yesu. Hili ni Fumbo linaloonesha historia ya ubinadamu, matumaini ya watu wa Mungu na Kanisa katika ujumla wake. Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni mwili na roho, anaendelea kuliombea Kanisa ambalo bado liko safarini, ili liweze kupata neema ya uzima wa milele. Bikira Maria kwa ulinzi na tunza yake ya kimama anaendelea kuwasindikiza watoto wa Kanisa ambao wako bondeni huku kwenye machozi, ili siku moja, waweze kufika mbinguni na kufurahia maisha na uzima wa milele. Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa mbinguni inakita mizizi yake katika imani, matumaini na mapendo yanayobubujika kutoka katika Fumbo la Umwilisho linalopata utimilifu wake katika Fumbo la Pasaka, yaani: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo Yesu kutoka kwa wafu. Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa mbinguni mwili na roho ni kielelezo cha ushindi wa nguvu ya upendo wa Mungu kwa waja wake.
Ilikuwa tarehe Mosi, Novemba 1950, katika Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu, Papa Pio XII katika Waraka wake wa Kitume “Munificentissimus Deus” yaani “Mungu Mkarimu” ndipo alipotangaza kwamba, “Bikira Maria, Mama wa Mungu ambaye daima ni Bikira, amepalizwa mbinguni mwili na roho baada ya kuhitimisha safari yake ya hapa duniani” kuwa ni Fundisho Tanzu la Imani ya Kanisa Katoliki. Hii ilitokana na sababu kwamba tangu mwanzo kabisa, Kanisa limekuwa linamwadhimisha Mama Bikira Maria kama Eva mpya huku akihusianishwa na Adamu mpya, yaani mwanae Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa maneno mengine, Sherehe hii inapata chimbuko lake katika Mapokeo ya Kanisa na hasa zaidi wakati wa Maadhimisho ya Mtaguso uliofanyika kunako mwaka 431 huko Efeso, Pwani Magharibi Asia ndogo Uturuki ya sasa. Ni Mtaguso huu ndio uliotamka kuwa Bikira Maria ni Mama wa Mungu, “Theotokos.” Bikira Maria ni Mama yake Kristo Yesu, ambaye ni Mwana wa Baba wa milele, Nafsi ya Pili katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Kanisa linaungama kweli kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Mungu. Tunapoadhimisha Sherehe hii, labda tujiulize ni kwa nini Mungu anampaliza mbinguni mwili na roho Mama yetu Bikira Maria? Kwa kifupi zipo sababu kubwa 4 zinazojibu swali letu: Bikira Maria anapalizwa mbinguni kwa sababu ni Mama wa Mungu Bwana Wetu Yesu Kristo kabla ya kutungwa mimba tumboni mwa Mama Bikira alikuwa na asili moja tu, yaani alikuwa ni Mungu tu. Injili ya Yohane inathibitisha ukweli huu: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu” (Yn. 1:1). Tangu Yesu anapotungwa mimba tumboni mwa Mama Bikira Maria anatwaa asili ya pili, yaani “anafanyika mtu” kwa kutwaa mwili wa kibinadamu kama Mwinjili Yohane anavyoeleza: “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu” (Yn. 1:14). Hivyo kwa kipindi chote cha miezi 9 alichokaa tumboni mwa Mama Bikira Maria (na milele yote) Bwana Wetu Yesu Kristo alikuwa na asili mbili: Ni Mungu na ni Mtu, hivyo Bikira Maria alimbeba na kumzaa Mungu-mtu. Kwa sababu hii Bikira Maria huitwa Mama wa Mungu pia (alimzaa Nafsi ya Pili ya Mungu katika ubinadamu). Loo! Ni heshima kubwa namna gani unastahili mwili wa mama huyu ambapo ndani mwake alikaa Mungu-mtu? Mwili wa Mama Yetu Bikira Maria ulikuwa ni mwili mtakatifu sana na uliotukuka sana kwani ulikuwa ni Mwili wa Mama wa Mungu.
Je, Mungu/Yesu angeweza kuruhusu mwili mtukuka wa Mama huyu kuoza kaburini? La hasha! Ndiyo maana aliamua kumpaliza mbinguni mwili na roho Mama huyu Mpendelevu sana ili mwili wake mtakatifu na mtukuka (mwili uliombeba na kumzaa Kristo Yesu, Nafsi ya Pili ya Fumbo la Utatu Mtakatifu katika mwili wa kibinadamu) usioze kaburini. Utangulizi wa Sherehe ya Kupalizwa mbinguni Bikira Maria unataja wazi kuwa alipalizwa mbinguni kwa kuwa ni Mama wa Mungu: “Nawe hukutaka kamwe aoze kaburini yeye aliyemzaa Mwanao, asili ya uzima wa vitu vyote.” Kumbe, kumzaa Kristo (kuwa Mama wa Mungu) ndiko kunamstahilisha Bikira Maria kupalizwa mbinguni. Mwili wake (na roho yake) unapalizwa mbinguni maana ni Mwili wa Mama wa Mungu mwili ambao katu haustahili kuozea kaburini. Bikira Maria alipalizwa mbinguni kwa sababu ni Mkingiwa dhambi ya asili na dhambi nyingine zote. Sababu hii tutaihusianisha pia na mapokeo/imani ya Wayahudi. Wayahudi waliamini kuwa mwili wa mtu mwenye dhambi huadhibiwa pia hata baada ya kufariki. Adhabu ambayo mwili wa mdhambi hupewa ni kuoza/kuharibika kwa mwili. Hivyo, kwa Wayahudi, kuoza kwa mwili ni kielelezo dhahiri kuwa mtu huyo alikuwa na dhambi na hivyo anaadhibiwa (mwili unaoza) kwa sababu ya dhambi zake. Ili kuonesha dhahiri kuwa Bikira Maria hakuwa na dhambi Mungu aliamua kumpaliza mbinguni mwili na roho ili mwili wake usioze/kuharibika kaburini, jambo ambalo lingemfanya aonekane kuwa alikuwa na dhambi na hivyo mwili unaadhibiwa. Hivyo Bikira Maria anapalizwa mbinguni ili kuthibitisha kuwa ni mkingiwa dhambi ya asili na dhambi nyingine zote.
Bikira Maria alipalizwa mbinguni mwili na roho kwa sababu ni Bikira daima. Mama yetu Bikira Maria ni bikira wa daima kabla ya kumzaa Yesu, wakati wa kumzaa Yesu na baada ya kumzaa Yesu alibaki kuwa Bikira. Alitunza ubikira wake usiharibiwe na mwanamume ili kujiweka wakfu kwa Mungu. Kwa kuwa alitunza ubikira wake daima yaani aliutunza mwili wake usiharibiwe na mwanamume kwa kuishi ubikira, Mungu naye alikusudia kuwa mwili wake usiharibiwe kaburini maana ulitunzwa vizuri kwa kiapo cha ubikira na ndiyo maana alimpaliza mbinguni mwili na roho ili azidi kuvitunza vizuri mwili na roho yake. Bikira Maria alipalizwa mbinguni mwili na roho kwa sababu alishiriki kazi ya ukombozi. Bwana Wetu Yesu Kristo alitukomboa kwa mateso makali, kwa kifo chake msalabani na ufufuko wake. Baada ya mateso hayo makali na kifo, Mungu Baba alimpa tuzo la ushindi: Alimfufua, kisha akapaa mbinguni na kuketi kuume kwa Baba yaani kutawala pamoja na Mungu Baba (Mdo. 7:56).
Kwa maneno mengi Yesu baada ya kumaliza kazi ya ukombozi alipewa tuzo na Mungu Baba (tuzo la kufufuka, kupaa mbinguni na kuketi kuume kwa Baba). Tuzo hili hakulipata bure bure- alilipata baada ya kumkomboa mwanadamu kwa mateso, kifo na ufufuko wake. Kadhalika, Bikira Maria alishiriki kazi ya ukombozi wa mwanadamu. Alishiriki vipi kazi ya ukombozi wamwanadamu? Kwanza, kwa kukubali kwake kumchukua mimba Bwana Wetu Yesu Kristo (kwa “fiat” yake. “Fiat” ni neno la Kilatini lenye maana ya “Nitendewe”); Pili, kwa kuteseka pamoja na mwanae. Hakuna anayepata mateso mengi kama mama anayeshuhudia mwanae akiteseka. “Atesekapo mtoto, mama naye huteseka.” Huu ni ukweli dhahiri. Mateso yote aliyopitia Yesu katika safari yake ya ukombozi wa mwanadamu yalimtesa vikali mama yake pia. Hivyo, Mama Bikira Maria alishiriki ukombozi wa wanadamu kwa kushiriki mateso ya mwanae, ingawa kwa namna tofauti. Kwa kuwa Mama Bikira Maria alishiriki kazi ya ukombozi, naye alistahili kupewa tuzo. Tuzo analopatiwa Bikira Maria si jingine bali ni kupalizwa mbinguni mwili na roho na kufanywa malkia mbinguni (Ufu. 12:1). Hivyo, Bikira Maria anapalizwa mbinguni kwa sababu alishiriki kazi ya ukombozi wa mwanadamu. Tumwombe Bikira Maria Malkia wa mbinguni, atusaidie ili sisi nasi tushirikishwe pia utukufu wa mwanaye. Amina.
