Askofu Msaidizi Vincent Lawrence Mpwaji, Jimbo kuu la Dar es Salaam, Tanzania
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV Jumamosi tarehe 11 Julai 2026 ameteuwa Mheshimiwa Sana Padre Vincent Lawrence Mpwaji wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, kuwa Askofu Msaidizi wa Jimbo kuu la Dar es Salaam. Itakumbukwa kwamba, Askofu Msaidizi Vincent Lawrence Mpwaji alizaliwa tarehe 5 Juni 1978, mjini Morogoro, nchini Tanzania. Mwaka 1993 alijiunga na Seminari Ndogo ya Visiga na kuhitimu mwaka 1996. Aliendelea na Masomo ya A Level Shule ya Sekondari Mazengo kuanzia mwaka1997 na kuhitimu mwaka 1999. Alijiunga na mwaka wa malezi, Kunduchi, Mtongani.Alipata masomo yake ya Falsafa kutoka Seminari kuu ya Mtakatifu Anthony wa Padua, Ntungamo, Jimbo Katoliki la Bukoba. Akaendelea na masomo yake ya Kitaalimungu, Seminari kuu ya Mtakatifu Karoli Lwanga, Jimbo kuu la Dar es Salaam. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi tarehe 7 Julai 2008 akapewa Daraja takatifu ya Upadre. Mwaka 2011 alitumwa na Jimbo kuu la Dar es Salaam kwenda Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian, kilichoko Roma na hapo akajipatia Shahada ya Uzamili- Umahiri katika Taalimungu na kuhitimu mwaka 2014. Kunako mwaka 2015 alitumwa tena kwenda kuongeza ujuzi na maarifa katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian na kuhitimu mwaka 2021 na hivyo kujipatia Shahada ya Uzamivu katika Taalimungu ya Mafundisho Sadikifu ya Kanisa.
Katika maisha na utume wake kama Padre amewahi kuwa Katibu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Katibu mtendaji wa Idara ya Elimu Jimbo kuu la Dar es Salaam. Wakili wa Mahakama ya Jimbo kuu la Dar es Salaam kati ya Mwaka 2008-hadi mwaka 2011. Baadaye alitumwa na Jimbo kuu la Dar es Salaam kwa masomo ya juu katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian kilichoko mjini Roma na mwaka 2021, akajipatia Shahada yake ya Uzamivu. Amewahi pia kuwa ni Mjumbe wa Kamati ya Miradi Jimbo kuu la Dar es Salaam kati ya Mwaka 2011 na tangu mwaka 2021 hadi kuteuliwa kwake na Baba Mtakatifu Leo XIV kuwa Askofu Msaidizi wa Jimbo kuu la Dar es Salaam alikuwa ni Chansela “Chancelor” wa Jimbo kuu la Dar es Salaam na Paroko-usu Parokia ya Kanisa kuu la Mtakatifu Yosefu, Jimbo kuu la Dar es Salaam. Askofu Msaidizi Mteule Vincent Lawrence Mpwaji, anawashukuru watu wote wa Mungu kwa kumwombea na kwamba, haya ni maajabu ya Mungu ambayo bado anaendelea kuyastajabia. Anawaomba watu watakatifu wa Mungu waendelee kumkumbuka katika sadaka na sala zao, ili aweze kutenda kadiri ya mapenzi ya Mungu mwenyewe.