Huduma ya kuoga,kwenye bafu zilizoko Mtakatifu Petro:Walio dhaifu wanapata hadhi!
Padre Łukasz Bankowski – Vatican.
Sr Hanna Kiedrowska wa Shirika la Wamisionari Wapalotini(SAC), lililoanzishwa na Padre Vicent Maria Palotti mwaka 1835 alitoa ushuhuda wa kugusa moyo kwa vyombo vya habari vya Vatican kuhusiana na watu wasio kuwa na makazi maalum jijini Roma. "Nilipokutana na vijana wasio na makazi kwa mara ya kwanza na kuwaita 'ndugu,' walitokwa na machozi. Waliniambia hakuna mtu aliyewahi kuwaita hivyo."
Tangu 2015, mtawa huyo wa Kipallottini kutoka Poland amekuwa akijitolea kwenye bafu zilizotengenezwa kwa ajili ya maskini na wasio na makazi zilizopo chini ya nguzo za Uwanja wa Mtakatifu Petro, mjini Vatican, mpango unaoendeshwa na Ofisi ya Baraza la Kipapa la Huduma ya Upendo. Kwa upande wa Sista huyo, alisisitiza kwamba jambo muhimu zaidi si kutoa msaada wa kimwili tu, bali kurejesha utu uliopotea wa watu.
. ![]()
Watawa na Walei wa kujitolea katika huduma ya Bafu zilizopo chini ya nguzo za Uwanja wa Mtakatifu Petro
Wanachohitaji zaidi ni mtu wa kuwasikiliza
Hata hivyo, msaada hauishii tu kwenye chakula na usafi. "Mara nyingi, wanataka kuzungumza tu" alielezea Sr Hanna. "Wanahitaji kuhisi kusikilizwa na kuulizwa ni nini kilichowafanya kuishi mitaani. Unapojifunza kuhusu historia yao, utoto wao, na hali ya familia, unaanza kuelewa ni majeraha mangapi wanayobeba ndani mwao." Sr aliongeza kusema kuwa watu wengi wanakabiliwa kunywa pombe au dawa za kulevya, lakini nyuma ya kila uraibu kuna historia halisi ya mateso."
"Hakuna mtu aliyewahi kutuita ndugu"
Mojawapo ya kumbukumbu zake kali zaidi tangu mwanzo wa huduma yake inahusisha kukutana na kundi la vijana wasio na makazi. "Nilikuwa nikipita chini ya handaki na niliwaita 'ndugu.' Wote walilia," alikumbuka mtawa wa Kipallottini"Waliniambia kwamba hakuna mtu aliyewahi kuwaita hivyo. Walisikia maneno makali na ya dharau. Ilikuwa wakati uliowagusa sana wao na mimi." Sr Hanna anaamini kwamba hata watu wanaoishi mitaani wanatafuta maana katika maisha yao na wanatamani kupata tena heshima yao, "lakini wengi wameumia sana," alisisitiza, "hivyo ni vigumu sana kwao kurudi kwenye maisha ya kawaida."
Kugundua upya hadhi ya Watoto wa Mungu
Sr Hanna anabainisha kwamba, kwa miaka mingi, ameelewa jinsi hata ishara rahisi zilivyo muhimu kwao. "Ninapokutana nao barabarani, ninasimama kila wakati, ninawasalimia, na kutabasamu. Pia alibainisha jinsi ilivyo muhimu kwao kuweza kuwaeleza waoge na kujitunza." "Hii inawasaidia kugundua tena hadhi yao kama watoto wa Mungu." Sr aliongeza kusema kuwa ni kutokana na huduma hiyo hasa amejifunza kutambua hadhi ya wengine kila siku: "Ninamshukuru Mungu kwa miaka hii kumi na moja ninayotumia kuwahudumia watu hawa. Siyo kazi rahisi, lakini kutokana nayo, nimeweza kuelewa vyema maisha yao na kushiriki maisha yao ya kila siku."
Lishe ya kiroho pia inahitajika
Sista huyo alisisitiza kwamba, pamoja na msaada wa kimwili, anahisi zaidi na zaidi hitaji la kusindikizana nao kiroho na watu wanaoishi mitaani. "Ningependa tuweze kukutana nao sio wakati wa kuoga au wakati wa kugawa chakula tu, bali pia katika sala," alielezea. "Tunahitaji nafasi ambapo tunaweza kuwaalika kuabudu Sakramenti Takatifu, kutafakari Neno la Mungu, au kushiriki nao katika Misa Takatifu. Safari ya malezi ya kiroho itakuwa utajiri mkubwa kwao." Sr Hanna alihitimisha kwa kukumbusha kwamba: "wanadamu hawahitaji mkate na paa juu ya vichwa vyao tu, bali pia kupata uzoefu wa upendo wa Mungu na kujisikia kuwa sehemu ya jumuiya ya Kanisa."
Imesasishwa tarehe 9 Julai 2026 saa 5.50 asubuhi na Angella Rwezaula.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.