Vatican yahimiza hatua kulinda maji na usafi wa mazingira Kimataifa
Na Sr. Christine Masivo, CPS - Vatican.
Mwakilishi wa kudumu wa Vatican katika ofisi za Umoja wa Mataifa, huko New York, Marekani akihutubia mnamo tarehe 7 Julai 2026, katika mjadala wa Kisiasa wa Ngazi ya Juu ya Umoja wa Mataifa kuhusu Lengo la 6 la Maendeleo Endelevu(SDG) na muunganisho wake wa lengo la Maendeleo Endelevu(SDG) kuhusu Maji na Usafi wa Mazingira, alihimiza lengo hilo liungwe mkono zaidi kwa nchi zinazoendelea na usimamizi wa kimaadili wa rasilimali maji.
Upatikanaji wa maji ni kipaumbele cha haki za binadamu na maendeleo
Mwakilishi wa Vatican alithibitisha tena kwamba, "upatikanaji wa maji na usafi wa mazingira salama ni muhimu kwa haki ya maisha na maendeleo endelevu." Akizungumza kuhusu Lengo la 6 la Maendeleo Endelevu(SDG6) alisisitiza kwamba, mabilioni ya watu wanaendelea kukabiliwa na upatikanaji duni wa maji safi na usafi wa mazingira, akielezea hali hiyo kama ukosefu wa usawa mkubwa wa Kimataifa. Pia alisisitiza kwamba "maji hayapaswi kuchukuliwa kama bidhaa ya kibiashara au rasilimali ya kiuchumi pekee yake, bali kama faida ya pamoja inayoshirikishwa na wanadamu wote." Alitoa "wito wa utawala unaozingatia usawa, mshikamano, na kanuni ya kuhakikisha rasilimali zinahifadhiwa kwa vizazi vya sasa na vijavyo."
Wito wa usimamizi wa maji wa kimataifa
Vatican ilihimiza "kuongezeka kwa usaidizi wa kifedha, uhamisho wa teknolojia, na mipango ya kujenga uwezo ili kusaidia nchi zinazoendelea kuboresha miundombinu ya maji na usafi wa mazingira." Mwakilishi wa Vatican kadhalika alisisitiza hali kwamba "kufikia lengo la Sita la Maendeleo Endelevu (SDG6) hakuhitaji suluhisho za kiufundi na kifedha tu, bali pia kujitolea kwa kiutamaduni na kimaadili kwa usimamizi wa maji unaowajibika."
Katika mjadala huo Mwalikishi wa Vatican alibainisha kwamba "umuhimu wa elimu na uelewa wa umma ili kuweza kuhimiza matumizi endelevu ya maji, kupunguza upotevu, na kuhamasisha matumizi yanayowajibika. Vatican ilitoa wito "kwa serikali kupitisha sera zinazowapa kipaumbele watu walio katika mazingira magumu na kuhakikisha upatikanaji sawa wa huduma za maji na usafi wa mazingira."Kwa mustakabali, Vatican ilisema kuwa "Mkutano ujao wa Maji wa tarehe 8 desemba 2026 ni fursa muhimu ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na kuharakisha maendeleo ya kufikia SDG6 na Malengo ya Maendeleo Endelevu yanayohusiana."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.